KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, December 4, 2013

KILI STARS YATINGA ROBO FAINALI KOMBE LA CHALENJI


Na Sophia Ashery, Nakuru
TANZANIA Bara, Kilimanjaro Stars imefuzu kucheza hatua ya robo fainali ya michuano ya soka ya Kombe la Chalenji, baada ya kuichapa Burundi bao 1-0.
Katika mechi hiyo iliyochezwa kwenye Uwanja wa Afrah mjini hapa, bao pekee na la ushindi la Kilimanjaro Stars lilifungwa na Mbwana Samata, anayecheza soka ya kulipwa katika klabu ya TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo.
Samata alifunga bao hilo dakika ya saba baada ya kuunganisha wavuni kwa kiki kali, mpira wa krosi uliopigwa na Salum Abubakar 'Sure Boy' kutoka pembeni ya uwanja.
Kwa matokeo hayo, Kilimanjaro Stars imemaliza mechi za kundi lake ikiwa na pointi saba na sasa itakutana na timu ngumu ya Uganda katika mechi ya robo fainali.
Kilimanjaro Stars ilianza kubisha hodi kwenye lango la Burundi dakika ya pili wakati Mrisho Ngasa alipoingia na mpira ndani ya mita 18, lakini shuti lake lilipanguliwa na kipa Arkazar Athur wa Burundi.
Kilimanjaro Stars ilifanya mashambulizi mengine mawili ya nguvu dakika ya 14 na 23, lakini shuti la Himid Mao lilimbabatiza beki mmoja wa Burundi na mpira kutoka nje wakati shuti la Thomas Ulimwengu liligonga mwamba wa goli kabla ya mpira kuokolewa na kipa Arthur wa Burundi.
Burundi nusura ipate bao dakika ya 27 wakati Ndikumana Yussuf alipopewa pasi na kubaki ana kwa ana na kipa Ivo Mapunda wa Kilimanjaro Stars, lakini shuti lake lilimlenga kipa huyo.
Kilimanjaro Stars ilijibu shambulizi hilo dakika ya 28 baada ya Samata kupewa pasi akiwa ndani ya eneo la hatari, lakini shuti lake lilimlenga kipa Arthur.
Sure Boy angeweza kuifungia bao Kilimanjaro Stars dakika ya 35 baada ya kupokea krosi maridhawa kutoka kwa Samata, akaingia na mpira ndani ya eneo la hatari la Burundi, lakini shuti lake lilitoka nje ya goli. Timu hizo zilikwenda mapumziko Kilimanjaro Stars ikiwa mbele kwa bao 1-0.
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi huku kila timu ikihaha kusaka bao. Katika mashambulizi hayo, Amri Kiemba alipata nafasi nzuri ya kuifungia bao Kilimanjaro Stars dakika ya 58, lakini shuti lake lilipaa juu.
Kilimanjaro Stars ilipata nafasi zingine nzuri za kufunga mabao dakika ya 76, 80 na 83, lakini mshuti ya Samata na Ulimwengu, aidha yaliishia mikononi mwa kipa Arhur ama kutoka nje ya lango.
Kili Stars: Ivo Mapunda, Erasto Nyoni, Himid Mao, Said Morad, Kelvin Yondan, Frank Domayo, Salum Abubakari, Mbwana Samata, Mrisho Ngasa, Thomas Ulimwengu na Amri Kiemba/Haruna Chanongo.
Burundi: Arakazar Athur, Hakizimana Issa, Hererimana Rashid, Nsabiyumva Fredrick, Nduwimana Jean, Ndikumana Yussuf,  Duhayinavyi Gael, Nduwarugira Christopher, Habonimana Celestin na Hussein Shabaan

No comments:

Post a Comment