KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, December 2, 2013

KASEJA ARIPOTI KAZINI YANGA



KIPA mpya wa klabu ya Yanga, Juma Kaseja ameanza rasmi mazoezi na timu hiyo kwa ajili ya kujiandaa kwa mzunguko wa pili wa michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara na klabu bingwa Afrika.

Kaseja alianza mazoezi hayo jana yaliyofanyika kwenye uwanja wa Bora ulioko Kijitonyama, Dar es Salaam, akisimamiwa na Kocha wa Makipa, Razack Siwa.

Hiyo ilikuwa mara ya kwanza kwa Kaseja kufanya mazoezi na Yanga baada ya kushindwa kufanya hivyo wiki iliyopita kutokana na kusumbuliwa na maumivu ya mkono.

Kipa huyo alisaliwa na Yanga mwezi uliopita, wakati wa usajili wa dirisha dogo, baada ya kuachwa na Simba msimu uliopita kwa madai ya kiwango chake kushuka.

Katika mazoezi ya jana, Kaseja alishirikiana na kipa mwingine wa zamani wa Simba, Ally Mustapha 'Barthez', ambaye tangu msimu uliopita, amekuwa kipa namba moja wa Yanga.

Hata hivyo, Barthez alipoteza namba yake kwenye kikosi cha Yanga baada ya timu hiyo kulazimishwa kutoka sare ya mabao 3-3 na Simba katika mechi ya mzunguko wa kwanza wa ligi kuu.

Nafasi hiyo kwa sasa inashikiliwa na Deogratius Munishi 'Dida', ambaye kwa sasa yuko na kikosi cha Tanzania Bara, kinachoshiriki michuano ya Kombe la Chalenji nchini Kenya.
 
Kocha Siwa alichukua muda mrefu kuzungumza na Kaseja na Barthez kabla ya kuanza kuwapa mazoezi ya pamoja.

Mazoezi hayo pia yalihudhuriwa na wachezaji wote wa Yanga, isipokuwa nyota wake watano walioko kwenye kikosi cha Tanzania Bara. Nyota hao ni Dida, Kelvin Yondan, Frank Domayo, Mrisho Ngasa, Athumani Iddi 'Chuji' na Simon Msuva.

No comments:

Post a Comment