KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, December 23, 2013

YANGA YAMTUPIA VIRAGO BRANDTS



KLABU ya Yanga imetangaza rasmi kumtimua kocha mkuu wa timu hiyo, Ernie Brandts pamoja na benchi lote la ufundi.

Uamuzi wa Yanga kumtimua kocha huyo umekuja siku chache baada ya timu hiyo kuchapwa mabao 3-1 na watani wao wa jadi Simba katika mechi ya Nani Mtani Jembe, iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya Yanga, Abdalla Ahmed Bin Kleb aliwaambia waandishi wa habari mjini Dar es Salaam jana kuwa, Brandts amepewa notisi ya mwezi mmoja kwa ajili ya kumaliza programu zake.
Bin Kleb alisema baada ya notisi hiyo kumalizika, kocha huyo atakuwa huru kwenda anakotaka.

Kwa mujibu wa Bin Kleb, sababu za kumuondoa kocha huyo ni kushuka kwa kiwango cha timu hiyo katika mechi za hivi karibuni na si kipigo cha Simba pekee.

“Kweli mwanzoni alipandisha kiwango cha timu, kilipanda sana, lakini baadaye kiwango kikaanza kushuka, tukasema tumpe muda kidogo, lakini tunaona mambo yanazidi kuharibika, hivyo tumeamua kuachana naye,”alisema.

Bin Kleb alisema utaratibu wa kuwaondoa maofisa wengine wa benchi la Ufundi unaendelea na kwamba, tayari mipango imeshaanza kufanyika kwa ajili ya kusaka kocha mpya.

Wakati huo huo, Yanga imethibitisha ushiriki wa timu hiyo katika michuano ya Kombe la Mapinduzi, inayotarajiwa kufanyika Januari mwakani visiwani Zanzibar.
Mbali na kushiriki katika michuano hiyo, Yanga pia inatarajia kufanya ziara ya mafunzo katika moja ya nchi za Ulaya.

No comments:

Post a Comment