KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, December 1, 2013

SIMBA SASA VURUGU TUPU, KOCHA MPYA, BERKO KUTAMBULISHWA LEO




KLABU ya Simba leo inatarajiwa kuwatambulisha rasmi kipa wake mpya,
Yaw Berko kutoka Ghana na Kocha, Zdravko Logarusic kutoka Croatia.

Ofisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga alisema jana kuwa, utambulisho huo utafanyika makao makuu ya klabu hiyo, mtaa wa Msimbazi, Dar es Salaam.

Kamwaga alisema, Logarusic, ambaye aliwahi kuifundisha Gor Mahia ya Kenya, ameletwa kwa ajili ya kuchukua nafasi ya Abdalla Kibadeni, ambaye amesimamishwa.

Kwa mujibu wa Kamwaga, baada ya utambulisho huo, Logarusic ataanza rasmi kukinoa kikosi cha Simba kwa ajili ya mzunguko wa pili wa ligi kuu ya Tanzania Bara, unaotarajiwa kuanza Januari mwakani.

Alisema Berko atatambulishwa akiwa kipa mpya wa Simba, kwa ajili ya mzunguko wa pili wa ligi kuu. Usajili wa dirisha dogo unatarajiwa kumalizika Desemba 15 mwaka huu.

Berko, aliwahi kuichezea Yanga misimu miwili iliyopita, lakini aliachwa kwenye usajili wa msimu huu kutokana na kushindwa kuelewana na viongozi wa klabu hiyo.
Kipa huyo ameletwa kuziba pengo la Juma Kaseja, ambaye amejiunga na Yanga.

Hata hivyo, ujio wa Logarusic na Berko huenda ukazua mtafaruku mwingine mkubwa Simba, kufuatia kuwepo kwa makundi mawili ya viongozi yanayopingana ndani ya Simba.

Awali, kamati ya utendaji ya Simba, ilitangaza kumsimamisha Mwenyekiti wa klabu hiyo, Ismail Aden Rage na makocha Kibadeni na msaidizi wake, Jamhuri Kihwelo, lakini mapinduzi hayo yalipingwa na Rage pamoja na Baraza la Wadhamini.

Baada ya kupinga mapinduzi hayo, Rage alitamka hadharani kuwa, Kibadeni ataendelea kuwa kocha mkuu wa timu hiyo.

Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), imemtaka Rage aitishe mkutano mkuu wa dharula wa wanachama ndani ya siku 14 ili kuzungumzia mgogoro huo na kuupatia ufumbuzi.

Lakini Rage amepinga agizo hilo la TFF na kusema kuwa, limekiuka katiba ya Simba na kumvua madaraka ya uenyekiti kwa vile mwenye mamlaka ya kuitisha mkutano mkuu ni mwenyekiti pekee.

No comments:

Post a Comment