KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, December 1, 2013

KILIMANJARO STARS YANUSA ROBO FAINALI



Frank Domayo (kushoto) na Ramadhani Singano 'Messi' wakimpongeza Haruna  Chanongo baada ya kuifungia bao pekee Kilimanjaro Stars dhidi ya Somalia jana katika mechi ya michuano ya Kombe la Chalenji, iliyochezwa kwenye Uwanja wa Nyayo mjini Nairobi. (Picha kwa hisani ya blogu ya Bin Zubeiry).

NA SOPHIA ASHERY, NAIROBI

TANZANIA Bara, jana ilijiweka kwenye nafasi nzuri ya kufuzu kucheza robo fainali ya michuano ya Kombe la Chalenji, baada ya kuichapa Somalia bao 1-0.

Katika mechi hiyo, iliyochezwa kwenye Uwanja wa Nyayo mjini hapa, Kilimanjaro Stars ilijipatia bao lake la pekee na la ushindi dakika ya 57 kupitia kwa mshambuliaji Haruna Chanongo.

Chanongo alifunga bao hilo baada ya kupokea pasi safi kutoka kwa Ramadhani Singano 'Messi'. Wote wawili waliingia kipindi cha pili kuchukua nafasi za Elias Maguli na Amri Kiemba.

Kwa ushindi huo, Kilimanjaro Stars sasa inazo pointi nne baada ya kucheza mechi mbili na inatarajiwa kutupa karata yake ya mwisho keshokutwa kwa kumenyana na
Burundi.

Pambano hilo lilianza kwa kasi ndogo huku kila timu ikiusoma mchezo wa mwenzake. Kilimanjaro Stars nusura ipate bao dakika ya tisa wakati Elias Maguli kupokea pasi safi kutoka kwa Mrisho Ngasa, lakini shuti lake lilitoka nje.

Somalia ilijibu shambulizi hilo dakika ya 16 wakati Jabir Hassan alipopewa pasi na kubaki ana kwa ana na kipa Ivo Mapunda, lakini shuti lake lilikwenda moja kwa moja mikononi mwa kipa huyo.

Kiungo Athumani Iddi 'Chuji' alifanyakazi nzuri dakika ya 21 na kumtengenezea chumba safi Ngasa, lakini shuti lake lilitoka nje.

Nafasi nyingine nzuri ya kufunga bao ilipotezwa na Kili Stars dakika ya 40 wakati Abubakar Salum alipotoa pasi safi ya juu kwa Said Morad, lakini mpira wa kichwa alioupiga, ulikuwa mboga kwa kipa Mohamed Sherrif wa Somalia. Timu hizo zilikwenda mapumziko zikiwa suluhu.

Somalia ilichachamaa dakika ya 71 na kufanya shambulizi kali kwenye lango la Kili Stars,  lakini shuti la Jabril Mohamed lilidakwa na kipa Mapunda.

Kili Stars: Ivo Mapunda, Himidi Mao, Erasto Nyoni, Saidi Moradm Kelvin Yondan, Frank Domayo, Abubakar Salum, Athumani Iddi, Mrisho Ngasa/Farid Mussa, Elias Maguli/ Ramadhani Singano 'Messi', Amri Kiemba/Haruna Chanongo.

Somalia: Mohamed Sherrif, Hassan Ali, Mohamed Shidane, Aden Hussein, Hassan Hussein, Daud Hassan, Sidi Mohamed, Mohamed Abdi, Jabril Hassan, Mohamed Saleh, Sadaq Abdulkadir.

No comments:

Post a Comment