KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, December 8, 2013

MESSI, RONALDO, RIBERY HAPATOSHI TUZO YA MWANASOKA BORA WA DUNIA 2013



MADRID, Hispania
 ALIANZA kwa utani, lakini hakuwa na maana
hiyo pale Rais wa Shirikisho la Soka Ulaya
(UEFA), Michel Platini, aliposema
waliongeza muda wa kupiga kura katika
mchakato wa kumpata mwanasoka bora wa
dunia, ili kumkosha Cristiano Ronaldo.
Baadaye, akadokeza tena kuwa, mchezaji wa
Hispania alistahili hasa kushinda tuzo ya
Ballon d'Or 2010 baada ya fainali za Kombe
la Dunia.
Hata hivyo, akashuka kwa kina kuwa, tuzo ya
kumpata mchezaji bora wa 2012/2013, ngumu
sana kwa sababu zinakutanisha wachezaji
mahiri ndiyo maana tabu kuchagua mshindi
kati yao.
Platini amesema kutokana na ugumu huo,tuzo
za safari hii zimeweka historia.
Wachezaji wanaominyana katika tuzo hiyo ni
Ronaldo wa klabu ya Real Madrid, Lionel
Messi wa Barcelona na Franck Ribery
anayekipiga Bayern Munich.
Messi aliisaidia Barcelona kutwaa ubingwa
wa Hispania 'La Liga' pamoja na kufunga
mabao matamu msimu uliopita, lakini Ronaldo
alikuwa msaada kwa Real Madrid, ingawa
hakupata nishani yoyote, wakati winga
Ribery aling'ara na Bayern Munich kwa
kuisaidia kubeba mataji matatu msimu wa
2012/2013.
Katika hayo, limo kombe la ligi ya mabingwa Ulaya.
Platini, ambaye aliwahi kunyakua tuzo ya
Ballon d'Or mara tatu, amesema hana
wasiwasi na kanuni za FIFA za kumpata
mchezaji mshindi.
Akasema kwa mzaha kuwa, muda wa kupiga kura
uliongezwa ili kumsafishia njia Ronaldo,
baada ya kuzozana hadharani na Rais wa FIFA
Sepp Blatter.
"Inavyoonekana Messi anawapiku Ronaldo na
Ribery," alisema.
"Wawili wa kwanza wanavutia na Ribery naye
ameshinda kila kitu.
"Ni wachezaji watatu walio bora. Kuchagua
mshindi wa Ballon d'Or mwaka huu ni ngumu
sana katika historia ya tuzo hii.
"Uamuzi wa kuongeza muda wa kupiga kura
ulikuwa wa FIFA, ingawa inaonekana chanzo
ni msukumo wa Ureno kufuzu Kombe la Dunia
kwa mabao matatu ya Ronaldo dhidi ya
Sweden,"alisema.
Aliongeza, huku anacheka: "Labda FIFA
imefanya hivi kumfurahisha Ronaldo."
Platini pia alishangaa kufuatia mchezaji wa
Hispania kukosa tuzo licha nchi hiyo kuwa
mabingwa wa dunia 2010, badala yake
Ballon d'Or ikaenda kwa Messi mara ya pili.
"Nashangaa kwa nini mchezaji wa Hispania
hakushinda," aliongeza Mfaransa huyo.
"Nakubali kuwa, mwaka 2010, tuzo ya Ballon
d'Or winner ilistahili kutwaliwa na
Mhispania.
"Andres Iniesta, Xavi na mwingine kwangu
mimi, mmojawapo alistahili kushinda. Messi
amenyakua ni bingwa mahiri. Lakini 2010,
tuzo ingekwenda kwa mchezaji kutoka Hispania."
Wakati hayo yakiendelea, bado kuna vita
kali kati ya Messi na Ronaldo kutokana na
wachezaji hao walivyochuana katika tuzo za
Hispania juzi.
Katika tuzo hizo, Ronaldo ameshinda ya
mchezaji mwenye thamani zaidi katika ligi
ya Hispania, huku Messi akitoka na 'zawadi'
mbili.
Messi amebeba tuzo ya mchezaji bora na
mshambuliaji bora wa ligi ya Hispania.
Angalau tuzo hiyo mpya ilimfurahisha
Ronaldo aliyekusanyika na wachezaji
mbalimbali na kupiga nao picha.
Miongoni mwa wachezaji hao ni mshambuliaji
wa Everton, Gerard Deulofeu, anayecheza kwa
mkopo katika timu ya daraja la pili, ambako
ameibuka mchezaji bora msimu uliopita na
kipa wa Chelsea, Thibaut Courtois
aliyeshinda tuzo ya kipa bora.Kipa huyo anacheza
kwa mkopo Atletico Madrid.
Kudhihirisha kuwa homa ya tuzo hiyo ni
kubwa, wachezaji mashuhuri wametoa maoni yao
na kila mmoja akimpigia kifua amtakaye!
Ronaldo de Lima jana alisema, anadhani Messi
anastahili kushinda tuzo hiyo na kuwapiku 
Ronaldo na Ribery.
Alisema haoni sababu ya nyota huyo wa
Argentina kutabiriwa kuwa mshindi wa tatu.
"Nafikiri Messi atanyakua tena Ballon d'Or,"
Ronaldo aliliambia gazeti la Marca.
"Messi amecheza mechi nyingi katika miaka
mitano iliyopita ni mchezaji nyota katika
ulimwengu wa soka. Sasa, majeraha yake si
makubwa sana, huenda mapumziko yakampa muda
wa kuchaji makali yake."
Ronaldo aliyewahi kucheza Barcelona na Real
Madrid kwa nyakati tofauti, alishinda tuzo
ya Ballon d'Or mara mbili, baada ya
kung'ara 1997 na 2002.
Kipa wa Real Madrid, Iker Casillas amesema
kwa kizazi cha sasa, hajaona mchezaji bora kuliko wote duniani
zaidi ya Ronaldo.
"Kuna mchezaji aliye mbele ya wenzake wote,
mwenye kiwango cha kushangaza na anayestahili sifa zote, huyu si mwingine
bali ni Cristiano Ronaldo," alisema
Casillas, ambaye ni nahodha wa Real Madrid.
"Sifikiri kama kuna shaka kuhusu hilo na
ameonyesha hivyo kutoka mechi moja hadi
nyingine katika timu ya Madrid ni tumaini
na tunamshukuru, miezi michache ijayo
tutafanikisha malengo yetu mwaka huu.”
Casillas anaamini Ronaldo anaweza
kukiongoza kikosi cha Carlo Ancelotti
kutwaa mataji matatu msimu huu.
Sherehe za kumpata mshindi wa tuzo hiyo
zitafanyika Januari 13 mwakani, ambapo mchakato wa
kupiga kura ulifungwa Novemba 29 baada ya
kuongezwa muda wa wiki mbili.

No comments:

Post a Comment