KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, December 4, 2013

YAYA TOURE: ASANTENI


LONDON, England
KIUNGO wa kimataifa wa Ivory Coast na klabu ya Manchester City ya England, Yaya Toure amewashukuru mashabiki kwa kumchagua kuwa mshindi wa tuzo ya mwanasoka bora wa Afrika ya BBC.

Toure (30), ambaye aliteuliwa kuwania tuzo hiyo kwa miaka minne mfululizo, alitangazwa kuwa mshindi juzi baada ya kuwabwaga wanasoka wenzake wanne waliofuzu kuingia fainali.

Wanasoka wengine waliokuwa wakiwania tuzo hiyo ni Pierre-Emerick Aubameyang, Victor Moses, John Mikel Obi na Jonathan Pitroipa.

"Asanteni mashabiki wote duniani, mnaoendelea kuniunga mkono. Hii inaonyesha ni kwa kiasi gani mashabiki wanakupenda na kuikubali kazi yako,"amesema kiungo huyo.

"Hiki ni kitu fulani maalumu kwa sababu si kura ya kocha, klabu au nahodha wa timu ya taifa. Ni kura za mashabiki,"aliongeza nyota huyo wa zamani, aliyewahi kuchezea klabu ya Barcelona ya Hispania.

"Siku zote, ni jambo linalofurahisha unapokuwa na mashabiki wengi nyuma yako. Nimefurahi kwa sababu tuzo hiyo nimepewa na mashabiki, nawashukuru sana,"anasema.

Toure anasema, alikuwa na kila sababu ya kushinda tuzo hiyo baada ya kuteuliwa kuiwania kwa miaka minne mfululizo.

Anasema kushinda tuzo hiyo kwake ni mafanikio makubwa, hasa ikizingatiwa kuwa, wanasoka alioshindana nao, wapo kwenye kiwango cha juu na wanacheza soka ya kimataifa.

"Nadhani pia kuwa, soka ya Afrika imekuwa ikipiga hatua kubwa kimaendeleo na hii ina maana kubwa kwetu. Nikiwa mwafrika, ninayo furaha kubwa," anasema Toure.

Uteuzi wa wanasoka walioteuliwa kuwania tuzo hiyo, ulifanywa na wataalamu 44 wa soka kutoka sehemu mbalimbali za Afrika. Vigezo vilivyozingatiwa katika uteuzi huo ni
akili, ufundi, ushirikiano na wachezaji wengine na nidhamu.

Mshindi wa tuzo hiyo, alipatikana kutokana na kura zilizopigwa na mashabiki kupitia mtandao wa BBC, aidha kwa njia ya simu au ujumbe wa maandishi.

Mashabiki wamempa Toure tuzo hiyo kutokana na kuiletea mafanikio makubwa Ivory Coast mwaka uliopita na pia kuonyesha uwezo mkubwa katika kucheza soka na kufunga mabao.

Mwaka 2013 haukuwa wa mafanikio makubwa kwa Toure kutokana na kutoshinda tuzo yoyote katika klabu ya Manchester City na Ivory Coast, lakini alionyesha kiwango cha juu katika kusakata kabumbu.

Baada ya kukatishwa tamaa kutokana na Manchester City kushindwa kutetea taji lake msimu uliopita, Toure amerejea uwanjani msimu huu kivingine, akiwa ameongeza kitu kipya katika uchezaji wake, kutokana na kuwa mahiri kwa ufungaji wa mabao ya mipira ya adhabu.

Toure alionyesha uwezo huo katika mechi ya ufunguzi wa ligi kuu ya England dhidi ya Newcastle kabla ya kufunga tena bao kwa staili hiyo katika mechi dhidi ya Hull. Ameshafunga mabao manne kwa staili hiyo, kati ya mabao saba aliyoifungia Manchester City.

Kwa mujibu wa rekodi, Toure amefunga mabao 13 hadi sasa kwa klabu yake hiyo pamoja na timu ya taifa ya Ivory Coast, ambayo ni ya kujivunia kwa mchezaji wa kiungo.

Uwezo huo wa Toure pamoja na uongozi wake, umeiwezesha Manchester City kushika nafasi ya nne katika msimamo wa ligi hiyo hadi sasa.

Toure pia alikuwa msaada kubwa katika kikosi cha Ivory Coast, kilichofuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia za 2014, zitakazofanyika nchini Brazil.

Ushindi huo ulikuwa faraja kubwa kwa Ivory Coast baada ya kuvurunda katika fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika, zilizofanyika mapema mwaka huu nchini Afrika Kusini baada ya kutolewa hatua ya robo fainali na Nigeria.

Nje ya uwanja, Toure amekuwa akiongoza mapambano ya kupinga vitendo vya ubaguzi wa rangi katika soka, baada ya kukumbwa na hali hiyo wakati wa mechi ya michuano ya ligi ya mabingwa wa Ulaya dhidi ya CSKA Moscow ya Russia.

Wafuatao ni washindi wa tuzo zilizopita za mwanasoka bora wa Afrika wa BBC:
•2012 - Christopher Katongo (Zambia & Henan Construction)
•2011 - Andre 'Dede' Ayew (Marseille & Ghana)
•2010 - Asamoah Gyan (Sunderland & Ghana)
•2009 - Didier Drogba (Chelsea & Ivory Coast)
•2008 - Mohamed Aboutrika (Al Ahly & Egypt)
•2007 - Emmanuel Adebayor (Arsenal & Togo)
•2006 - Michael Essien (Chelsea & Ghana)
•2005 - Mohamed Barakat (Al Ahly & Egypt)
•2004 - Jay Jay Okocha (Bolton & Nigeria)
•2003 - Jay Jay Okocha (Bolton & Nigeria)
•2002 - El Hadji Diouf (Liverpool & Senegal)
•2001 - Sammy Kuffour (Bayern Munich & Ghana)
•2000 - Patrick Mboma (Parma & Cameroon)

No comments:

Post a Comment