KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, April 18, 2012

JUA CALI: Muziki umeniwezesha kumiliki studio



MSANII nyota wa muziki kutoka Kenya, Jua Cali amesema fani hiyo imemwezesha kupata manufaa mengi kimaisha, ikiwa ni pamoja na kumiliki studio yake mwenyewe.
Mbali na kujenga studio, Jua Cali amesema muziki umemwezesha kupata pesa nyingi na kuwasaidia watu kadhaa wenye matatizo.
Jua Cali alisema hayo hivi karibuni alipokuja kufanya onyesho la pamoja na msanii Juma Kassim ‘Nature’ lililofanyika kwenye ukumbi wa Dar Live mjini Dar es Salaam.
“Ukiuheshimu muziki na kufanyakazi kwa kujituma, utaweza kupata mafanikio makubwa kimaisha,”alisema msanii huyo, ambaye ni kipenzi cha walala hoi nchini Kenya.
Jua Cali alisema kwa sasa anakaribia kukamilisha ujenzi wa nyumba yake na hayo yote yametokana na kazi ya muziki.
Kwa sasa, Jua Cali anatamba kwa kibao chake kipya kinachojulikana kwa jina la Genge, ambacho kimekuwa kikishika chati za juu kwenye vituo mbalimbali vya redio na televisheni nchini Kenya.
Akizungumzia muziki wa bongo fleva, Jua Cali alisema anavutiwa na msanii Nature kutokana na nyimbo zake kuwa na mvuto na pia kukubalika na mashabiki wa hali ya chini.
“Nampenda sana Juma Nature kwa sababu nyimbo zake zinawagusa sana watu wa maisha ya chini na anakubalika sana Bongo. Na mimi nakubalika sana Kenya kwa sababu hiyo hiyo,”alisema.
Alipoulizwa kuhusu madhumuni ya onyesho lake na Nature, alisema halikuwa na lengo la kutafuta pesa zaidi ya kuwapa burudani mashabiki.
Jua Cali alisema bado hajafunga ndoa na wala hana mtoto. Alisema anaye mchumba na wanatarajia kufunga ndoa hivi karibuni.

No comments:

Post a Comment