KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, April 18, 2012

MARUFUKU KUMTEMBELEA LULU MAHABUSU

JESHI la Magereza nchini limepiga marufuku watu wasiokuwa na uhusiano na msanii chipukizi wa filamu nchini, Elizabeth Michael ‘Lulu’ kumtembelea katika mahabusu ya Segerea.
Lulu anashikiliwa katika gereza hilo kwa tuhuma za mauaji ya msanii nyota wa filamu nchini, Steven Kanumba baada ya kufikishwa mahakamani kwa mara ya kwanza wiki iliyopita.
Habari zilizotangazwa na kituo cha Radio One jana zilieleza kuwa, kwenye ubao wa matangazo ndani ya gereza hilo, kumeandikwa barua inayotoa maelekezo kuhusu watu wanaopaswa kumuona Lulu.
Kwa mujibu wa barua hiyo, watu wanaopaswa kumtembelea Lulu kwenye mahabusu hiyo ni mama yake mzazi, dada yake na mjomba wake, ambao picha zao zimebandikwa kwenye ubao huo wa matangazo.
“Watu wamezusha sana maneno kuwa, askari wamepiga marufuku hakuna mtu yeyote kumtembelea Lulu, ni uzushi tu,” alisema mmoja wa watangazaji wa kipindi hicho aliyetembelea kwenye mahabusu hiyo juzi.
Lulu anatuhumiwa kuhusika na kifo cha Kanumba, aliyefariki usiku wa kuamkia Aprili 7 na mazishi yake kufanyika Aprili 10 mwaka huu. Alifikishwa kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi ya Kisutu kwa mara ya kwanza wiki iliyopita na kesi yake itatajwa tena Aprili 23 mwaka huu.
Wakati huo huo, upande wa mashitaka katika kesi ya kutakatisha fedha haramu inayomkabili msanii maarufu wa filamu nchini, Kajala Masanja na mumewe Faraji Chambo inatarajiwa kuwa na mashahidi 13 na vielelezo tisa.
Kajala na Chambo walipandishwa kizimbani jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam mbele ya Hakimu Mkazi, Sundi Fimbo.
Wakili wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (PCCB), Leonard Swai alidai kesi hiyo ilifikishwa mahakamani hapo kwa ajili ya kuwasomea maelezo ya awali washitakiwa hao.
Katika maelezo hayo, washitakiwa walikubali baadhi ya mambo kuwa ni mume na mke, waliuza nyumba kwa Emiliana Regarulila na Chambo alikubali alikuwa ni mtumishi wa benki ya NBC mwaka 2008.
Washitakiwa walikataa kupewa notisi na Mwanasheria Mkuu wa Serikali wasiuze nyumba hiyo kwa sababu ilikuwa kwenye uchunguzi, hawakwenda kinyume na notisi hiyo na kumuuzia nyumba Emiliana.
Mambo mengine waliyokataa ni kwamba hawakuhamisha nyumba hiyo kwa Emiliana kwa kutumia fedha za rushwa.
Swai alidai wanatarajia kuwa na mashahidi hao na vielelezo hivyo na Hakimu Mkazi Sundi alisema kesi hiyo itaanza kusikilizwa Aprili 30, mwaka huu.

No comments:

Post a Comment