KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, January 5, 2012

FLAVIANA: Sipendi kuitwa mrembo


MWANAMITINDO wa kimataifa wa Tanzania, Flaviana Matata amesema hafurahii kuitwa mrembo kwa sababu kazi yake ni tofauti na fani hiyo.
Flaviana (25), ambaye aliwahi kutwaa taji la Miss Universe Tanzania mwaka 2007, alisema hayo wiki hii kupitia kipindi cha Mkasi kilichorushwa hewani na kituo cha televisheni cha Channel Five.
Alisema kazi ya uanamitindo imempa heshima na thamani kubwa kwa vile anaweza kwenda popote na kusikilizwa, tofauti na wasichana wengine waliowahi kushiriki mashindano ya urembo.
Mwanadada huyo alisema wanamitindo waliopo sasa Tanzania wanajiharibia wenyewe kutokana na kutokuwa makini na kazi yao na pia kutojiheshimu.
Binti huyo maridhawa aliwaponda wabunifu wa mavazi wa Tanzania kuwa, hawawalipi wanamitindo wao inavyotakiwa, badala yake wamekuwa wakiwatumia kujinufaisha.
“Wabunifu hawawalipi wanamtindo wao ndio sababu mimi binafsi hatuelewani. Wengine wanawalipa wanamitindo sh. 50,000 wakati pesa wanazopata ni nyingi.
“Kuna siku niliwahi kuwaeleza baadhi ya wanamitindo bajeti ya wabunifu wa mavazi, lakini wengine hawakujali, pengine kwa sababu wanapenda kuuza sura,”alisema mwanamitindo huyo mwenye makazi yake nchini Marekani hivi sasa.
Flaviana alisema dawa pekee ya kupambana na wabunifu wa aina hiyo ni kuwagomea, lakini alieleza kusikitishwa kwake kuona kuwa, wanamitindo wa Tanzania hawana umoja.
“Hapa naona cha msingi ni wewe binafsi kuwa na msimamo,”alisema Flaviana, ambaye alishiriki shindano la dunia la Miss Universe mwaka 2007 na kuingia hatua ya 15 bora na kushika nafasi ya sita.
Mwanamitindo huyo alisema wapo baadhi ya wabunifu wa mavazi na wanamitindo wanaomuona anaringa kutokana na mafanikio yake, lakini alisema hivyo sivyo alivyo.
“Hata kama najidai, nina haki ya kufanya hivyo kwa sababu hakuna hata mtu mmoja aliyewekeza pesa zake kwangu, lakini wapo walionipa moyo na kuniunga mkono katika kazi hiyo,”alisema.
Mwanadada huyo mwenye mwili mwembamba mithili ya mtu asiyependa kubugia msosi kwa wingi alisema, mafanikio yake katika fani hiyo yametokana na kujiamini kwake na kufanyakazi kwa bidii.
Alieleza kusikitishwa kwake kuona kuwa, wanawake wengi wa Tanzania wanashindwa kupongezana na kupeana moyo katika mafanikio, badala yake hawapendani.
Alisema kupitia mtandao wa facebook, amekuwa akipata maoni mengi kutoka kwa wanaume kuhusu kazi yake hiyo ya uanamitindo kuliko wanawake wenzake.
Alipoulizwa kuhusu uhusiano wa kimapenzi, Flaviana alisema kwa sasa hana rafiki yoyote wa kiume kwa vile hapendi kukutwa na madhila yaliyompata miaka kadhaa iliyopita.
Alikiri kuwa, wapo wanaume wengi waliowahi kumtongoza, lakini hapendi kuwa na uhusiano wa kimapenzi kwa sasa kwa kuhofia kukutwa na yaliyowahi kumkuta.
Flaviana alisema mwili wake hautokani na kujinyima kula ama kufanya mazoezi gym, bali hayo ni maumbile yake aliyozaliwa nayo.
“Mimi kamwe sijikondeshi, huu ni mwili wangu. Kama ni kula chakula, nakula sana, sijawahi kufanya mazoezi gym hata siku moja,”alisema.
Akizungumzia taasisi yake aliyoianzisha mwanzoni mwa mwaka jana, Flaviana alisema imelenga kutoa misaada ya aina mbalimbali kwa watu wenye matatizo.
Alisema kupitia taasisi yake hiyo, ameamua kuwasomesha watoto 10 wa kike katika shule za sekondari kutokana na wazazi wao kutokuwa na uwezo wa kufanya hivyo.
Flaviana alisema iwapo Mungu ataendelea kumuweka hai, anataka kuona watoto hao wanamaliza shule na kufanyakazi ili waweze kujitegemea kimaisha.
Flaviana alizaliwa Juni 1987. Mama yake alifariki katika ajali ya meli ya MV Bukoba iliyotokea mwaka 1996.
Licha ya picha yake kutumika kutangaza vipodozi vya Sherri Hill, mwanadada huyo aliwahi kushinda tuzo ya mwanamitindo bora wa mwaka 2011 kupitia jarida la Arise la Nigeria.
Picha za mwanadada huyu pia zimewahi kutumika kupamba majarida ya Dazed & Confused, Glass na ID ya Marekani. Pia amewahi kuonyesha mavazi ya wanamitindo maarufu duniani kama vile Vivienne Westwood, Tory Burch, Suno na Louise Gray.

No comments:

Post a Comment