KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, January 5, 2012

PAPIC: Sina bifu na viongozi wa Yanga


SWALI: Hivi karibuni ulikaririwa ukisema kuwa upo kwenye wakati mgumu kutokana na wewe binafsi na wachezaji wako kukosa mishahara kwa miezi kadhaa. Je, uongozi wa Yanga umeshalitafutia ufumbuzi tatizo hilo? Na nini hatma yako Yanga?
JIBU: Mwanzoni niliamua kuvumilia, lakini baada ya kukabiliana nalo kwa muda mrefu, nimeamua kuweka mambo hadharani kwa wanachama na wadau wote wa Yanga ili waweze kufahamu ukweli wa mambo.
Mbali na kucheleweshewa mshahara, nyumba niliyopangiwa na Yanga ina matatizo makubwa, ikiwa ni pamoja na kukatwa kwa huduma ya maji na umeme.Huduma hizo hazipatikani nyumbani kwangu.
Lakini kwangu hayo naona ni matatizo ya kawaida. Kikubwa ni kwamba nilijisikia vibaya baada ya mimi na wachezaji wangu kukosa mishahara kwa miezi miwili. Hili liliwavunja nguvu sana wachezaji.
Hebu fikiria, mtu mwenye familia anakosa mishahara kwa miezi miwili na mbele yake kuna sikukuu za Krismas na mwaka mpya. Unadhani mtu huyu ataweza kufanyakazi kwa kujituma? Haiwezekani.
Atakachokifanya ni kutafuta mahali, ambako anaweza kwenda kuomba msaada ama kukopa pesa ili aweze kujikimu.
Hivyo napenda kuweka wazi kuwa, sina ugomvi na kiongozi yeyote wa Yanga, isipokuwa nataka kuweka mambo sawa ili huko mbele nisije kulaumiwa mimi kwa kuonekana sifai wakati tatizo ni la uongozi.
SWALI: Baada ya kuzungumza na viongozi wa Yanga, mambo yakoje? Huoni kwamba kauli yako hiyo inaweza kujenga chuki kati yako na viongozi?
JIBU: Hapana, sidhani kama itakuwa hivyo. Kwa sasa nasubiri kikao cha kamati ya utendaji, ambacho kitajadili tatizo lililojitokeza ikiwa ni pamoja na kutafuta suluhisho.
Na kama itatokea viongozi wa Yanga kunichukia, watakuwa wamefanya kosa kwa vile sioni ubaya nilioufanya. Nilichokifanya ni kueleza ukweli wa mambo.
Lakini bado nina imani na viongozi wa Yanga kwamba wataweza kujipanga vizuri na kuwalipa wachezaji mishahara ili waweze kuwa na ari ya kuitumikia timu yao.
SWALI: Binafsi upo tayari kujiuzulu iwapo hali itaendelea kuwa ngumu kwako na kwa wachezaji?
JIBU: Sidhani kama jambo hilo linaweza kutokea kwa sababu Yanga ni klabu kubwa na inao wanachama na wapenzi wengi wenye uwezo wa kuisaidia kifedha.
Ninavyojua ni kwamba, kwa sasa uongozi upo kwenye mikakati ya kutafuta pesa kutoka kwa wafadhili na watu mbalimbali ili uweze kuiweka timu kambini na kuwahudumia wachezaji.
Kwa sasa, sipendi kuzungumzia jambo hilo kwa undani zaidi. Ninachoweza kusema ni kwamba mimi bado ni kocha wa Yanga na nitaendelea kuwepo hapa. Napenda kuiona timu yangu ikifanya vizuri katika michuano ya klabu bingwa Afrika.
SWALI: Unawaeleza nini wana Yanga kuhusu matatizo yaliyojitokeza katika klabu yao.
JIBU: Nawaomba viongozi na wanachama wawe makini katika maandalizi ya michuano hii kwa sababu ni mikubwa na timu tuliyopangwa kuanza nayo (Zamalek) ni ngumu.
Mashindano hayo ni makubwa na yana faida mbili za msingi, ikiwemo kupata pesa nyingi endapo tutafuzu kucheza hatua ya makundi ama kuibuka mabingwa wa Afrika.
Pia baadhi ya wachezaji wanaweza kupata ofa kutoka timu za nje na kununuliwa iwapo wataonyesha viwango vya juu na hivyo klabu kunufaika kipesa.
Kwa maana hiyo, ni vyema tukawekeza nguvu kubwa katika kujiandaa na mashindano hayo ili lengo hilo au ndoto tuliyonayo iweze kutimia.
Lakini pia bado tunakabiliwa na changamoto kubwa ya kutetea ubingwa wetu wa ligi kuu ya Tanzania Bara.
Wasiwasi wangu ni kwamba, iwapo uongozi utazembea kutatua matatizo yaliyopo sasa, ari ya wachezaji itashuka na hivyo tutashindwa kufanya vizuri katika mashindano yanayotukabili.
SWALI: Je, umeshapata taarifa zozote kuhusu timu ya Zamalek ya Misri, ambayo mnatarajiwa kupambana nayo mwezi ujao?
JIBU: Taarifa nilizonazo hadi sasa kuhusu Zamalek ni chache na nimezipata kupitia mitandao mbalimbali. Lakini bado naendelea kuwasiliana na viongozi wa kamati ya mashindano ya Yanga ili tuweze kupata taarifa nyingi zaidi na pia kujipanga kukabiliana nayo.
SWALI: Unazungumziaje michuano ya Kombe la Mapinduzi iliyoanza wiki hii huko Zanzibar. Je, kuna matumaini yoyote kwa timu yako kufanya vizuri?
JIBU:Nilichopanga ni kuyatumia mashindano hayo kupima uwezo wa wachezaji na pia kujiandaa kwa mzunguko wa pili wa ligi kuu na mechi yetu dhidi ya Zamalek. Hakuna lingine zaidi ya hayo.

No comments:

Post a Comment