KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, July 5, 2013

KIGOMA HOI KWA KINONDONI



Mchezaji wa timu ya soka ya wanawake ya Ilala, Zuena Azizi (kushoto) na Neema Paul wa Temeke wakigombea mpira wakati timu hizo zilipomenyana katika mechi ya michuano ya Kombe la Airtel Rising Star iliyochezwa jana kwenye uwanja wa Karume, Ilala, Dar es Salaam.  Ilala ilishinda kwa penalti 2-0. (Picha na Abubakari Habibu wa A3 Institute of Professional Studies).

NA MKUNDAPAI ABDALLAH
TIMU ya soka ya wanawake ya vijana wa chini ya miaka 17 ya Kigoma jana ilipata kichapo cha mabao 7-0 kutoka kwa Kinondoni katika mechi ya michuano ya Kombe la Airtel Rising Star iliyochezwa kwenye Uwanja wa Karume, Ilala, Dar es Salaam.

Katika mechi hiyo ya nusu fainali,  mshambuliaji Sherida Boniface ndiye aliyeibeba Kinondoni baada ya kuifungia mabao manne kati ya saba. Alifunga mabao hayo dakika za 10, 14, 26 na 38.

Mabao mengine ya Kinondoni yalifungwa na Tatu Iddi dakika ya sita, Shamimu Hamisi dakika ya 23 na Cristina Daudi dakika ya 40.

Kutokana na ushindi huo, Kinondoni sasa itakutana na Ilala katika mechi ya fainali. Ilala ilifuzu kucheza hatua hiyo baada ya kuichapa Temeke mabao 2-0. Temeke na Kigoma zitakutana katika mechi ya kutafuta mshindi wa tatu.

Pambano kati ya Ilala na Temeke lilikuwa na ushindani mkali na ilibidi mshindi apatikane kwa njia ya matuta baada ya timu hizo kumaliza dakika 90 zikiwa sare ya bao 1-1.

Temeke ilikuwa ya kwanza kupata bao dakika ya 32 kupitia kwa Neema Paul kabla ya Ilala kusawazisha dakika ya 50 kupitia kwa Donisia Daniel.

Katika kupigiana penalti tano tano, Ilala ilipata penalti mbili wakati Temeke ilipoteza tatu.


No comments:

Post a Comment