KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, July 10, 2013

HAKUNA HILA KWENYE MAREKEBISHO YA KATIBA-TENGA



Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga amesema hakuna hila yoyote katika marekebisho ya Katiba kwa vile yametokana na maagizo ya Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA).

Akizungumza na Wahariri wa Michezo kwenye ofisi za TFF, Dar es Salaam leo (Julai 9 mwaka huu), Rais Tenga amewahakikishia wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Dharura kuwa dhamira ya marekebisho hayo ni nzuri, kwani lengo ni kila mtu apate haki yake.

Amesema Mkutano huo utakaofanyika Jumamosi (Julai 13 mwaka huu) utakuwa na ajenda moja tu ya kuingiza Kamati ya Maadili, na Kamati ya Rufani ya Maadili katika Katiba ya TFF kama ilivyoelekezwa na FIFA ili baadaye uanze mchakato wa uchaguzi.

“Katika kuunda Kamati ya Maadili tumeangalia ile ile ya FIFA, tusitengeneze kitu kipya, yaondolewe yale yanayotakiwa kuondolewa, na yaongezwe yale yanayotakiwa kuongozwa. Kwa sababu tumeangalia mazingira kwa Tanzania ni tofauti na Ujerumani au nchi za sehemu zingine,” amesema.

Rais Tenga amewataka wajumbe wafike kwenye Mkutano wakiwa na mtazamo wa kujenga, kwani kuna maagizo ya FIFA ambayo wanatakiwa kuyatekeleza ili wasonge mbele.

“Tutawaeleza kwanini hili limewekwa na lile limeondolewa. Mpira unataka unit (kitu kimoja), ni mchezo wa kila mtu. Baada ya hapa tunaanzisha mchakato wa uchaguzi. Watu wanaingia wakiwa wamoja, wanatoa hoja wanasikilizwa. Wanahukumiwa kwa hoja,” amesema na kuongeza utatolewa muda wa kutosha wajumbe ili wayaone na kuelewa marekebisho hayo.

Rais Tenga pia alizungumzia kipindi hiki cha usajili na kutaka klabu ziwaachie wataalamu wa mpira wa miguu kwani ndiyo wanaojua upungufu wa timu, hivyo wanaweza kusajili wachezaji sahihi.
Amesema tatizo kubwa la klabu za Tanzania ni kuwa timu zao hazina uwezo wa kuhimili dakika 90, hivyo watu wanapaswa pia kuzungumzia aina ya mazoezi ambayo timu zao zinafanya badala ya kubakia kutaja tu majina ya wachezaji wanaotaka kusajiliwa.

KIINGILIO MECHI YA STARS, UGANDA 5,000/-
Kiingilio cha chini katika mechi ya mchujo ya Kombe la Afrika kwa Wachezaji wa Ligi za Ndani (CHAN) kati ya Tanzania (Taifa Stars) na Uganda (The Cranes) itakayochezwa Jumamosi (Julai 13 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam ni sh. 5,000 kwa viti vya rangi ya kijani.

Viti vya kijani katika uwanja huo wenye uwezo wa kuchukua watazamaji 60,000 viko 19,648. Kwa upande wa viti vya rangi ya bluu ambavyo viko 17,045 kiingilio ni sh. 7,000. Kiingilio kwa viti vya rangi ya chungwa ambavyo viko 11,897 ni sh. 10,000.

Viingilio vya daraja la juu ni kama ifuatavyo; VIP C yenye watazamaji 4,060 ni sh. 15,000 wakati sh. 20,000 ni kwa VIP B yenye watazamaji 4,160. VIP A yenye watazamaji 748 kiingilio chake ni sh. 30,000.

Mechi hiyo ya kwanza ya raundi ya mwisho kuwania tiketi ya kucheza fainali hizo zitakazofanyika mwakani nchini Afrika itachezeshwa na mwamuzi Thierry Nkurunziza kutoka Burundi. Mechi ya marudiano itachezwa jijini Kampala kati ya Julai 26 na 28 mwaka huu.

Tiketi kwa ajili ya mechi hiyo itakayoanza saa 9 kamili alasiri zitaanza kuuzwa siku moja kabla ya mchezo (Ijumaa) katika vituo vifuatavyo; Shule ya Sekondari Benjamin Mkapa, Sokoni Kariakoo, mgahawa wa Steers ulioko mtaa wa Ohio/Samora, Oilcom Ubungo, Kituo cha Mafuta Buguruni, Dar Live Mbagala na BMM Barbershop iliyoko Sinza Madukani.

Katika vituo hivyo tiketi zitauzwa katika magari maalumu. Magari hayo pia yatafanya mauzo ya tiketi uwanjani siku ya mechi.

Tunapenda kuwakumbusha watazamaji kutonunua tiketi mikononi mwa watu au katika maeneo yasiyohusika ili kuepuka kununua tiketi bandia, hivyo kukosa fursa ya kushuhudia mechi hiyo.

MIKOA YATAKIWA KUWASILISHA RATIBA COPA COCA-COLA
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), linavitaka vyama vya mpira wa miguu vya mikoa kuwasilisha ratiba zao za michuano ya U15 Copa Coca-Cola kabla ya Julai 15 mwaka huu.

Ni vyama vya mpira wa miguu vya mikoa 16 pekee ambavyo ndivyo vimewasilisha TFF ratiba hizo mpaka sasa. Jumla ya mikoa 32 ya Tanzania Bara na Zanzibar inashiriki katika michuano hiyo ya umri chini ya miaka 15 kuanzia ngazi ya wilaya ambapo ngazi ya mikoa inatakiwa kuanza Julai 15 mwaka huu.

Mikoa ambayo tayari imewasilisha ratiba zao ni Arusha, Ilala, Kagera, Kaskazini Pemba, Kaskazini Unguja, Kigoma, Kinondoni, Kusini Pemba, Kusini Unguja, Manyara, Mara, Mjini Magharibi, Morogoro, Singida, Tanga na Temeke.

WASH UNITED YAKABIDHI FULANI 200 KWA KLINIKI YA TFF
Taasisi ya Wash United inayojishughulisha na usaji na utunzaji mazingira imeikabidhi fulana 200 na dola 1,000 za Marekani kwa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa makubaliano kati yake na TFF yaliyosainiwa Novemba mwaka jana.

Fulana hizo kwa ajili ya kliniki za kila wikiendi (Jumamosi na Jumapili) zinazoendeshwa na TFF katika vituo 20 nchini kikiwemo cha Karume ikiwa ni sehemu ya mpango wa grassroots unaoshirikisha watoto wa umri kati ya 6 na 17 zimekabidhiwa na Mratibu wa Wash United, Femin Mabachi.

Hafla ya kukabidhi msaada huo imefanyika leo (Julai 9 mwaka huu) kwenye ofisi za TFF ambapo kwa upande wake ulipokelewa na Ofisa Maendeleo wake Salum Madadi.

Wash United inafadhiliwa na Serikali ya Ujerumani kupitia shirika lake la maendeleo la GIZ, na hapa nchini moja ya eneo wanalotumia katika kampeni hiyo ili kupambana na magonjwa kama kuhara yanayosababishwa na uchafu ikiwemo kutonawa mikono vizuri, hivyo kusababisha vifo kwa Watanzania ni mpira wa miguu.

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF

No comments:

Post a Comment