KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, July 3, 2013

NGASA AWEKA MAMBO HADHARANI

MSHAMBULIAJI Mrisho Ngasa wa klabu ya Yanga ameahidi makubwa kwa mashabiki wa klabu hiyo wakati atakapoanza kuichezea katika msimu ujao wa michuano ya soka ya ligi kuu ya Tanzania Bara.

Ngasa amesema atahakikisha anawarejeshea fadhila mashabiki wa klabu hiyo kutokana na kumuunga mkono alipokuwa akizichezea timu za Simba na Azam.


Mshambuliaji huyo nyota wa timu ya Taifa, Taifa Stars alisema hayo juzi aliporipoti kwa mara ya kwanza katika mazoezi ya Yanga yaliyofanyika kwenye uwanja wa shule ya msingi ya Loyola, Dar es Salaam.

"Ninawahakikishia mashabiki wa Yanga kwamba mimi ni mchezaji halali wa timu yao na sina deni lolote na Simba kwa vile nilishamaliza mkataba wangu,"alisema mshambuliaji huyo, ambaye alikuwa wa kwanza kuripoti mazoezini.

Ngasa aliihama Yanga miaka mitatu iliyopita na kujiunga na Azam kwa uhamisho uliogharimu sh. milioni 50 kabla ya kuuzwa kwa mkopo kwa klabu ya Simba.

"Naipenda sana Yanga. Nilikwenda Azam na Simba kwa ajili ya kutafuta maisha. Nitawadhihirishia mashabiki wa Yanga kwamba kiwango changu bado kipo juu,"alisema mshambuliaji huyo.

Ngasa alisema atakapoanza kuichezea Yanga katika michuano ya ligi na kimataifa, atahakikisha anakuwa mpishi mzuri wa mabao na pia mfungaji.

Aliwasifu washambuliaji Didier Kavumbagu na Saidi Bahanuzi kwamba ni washambuliaji wazuri na kusisitiza kuwa, uwepo wake utawafanya wazidi kung'ara.

"Inawezekana Kavumbagu na Bahanuzi walikosa mpishi mzuri wa mabao, lakini sasa wamempata, washindwe wenyewe. Hakutakuwa na sababu ya kutafuta mchawi,"alisema.

Ngasa alisifu usajili uliofanywa na benchi la ufundi la Yanga kwa ajili ya msimu ujao wa ligi na kuongeza kuwa, ana hakika wanaweza kutwaa ubingwa mapema zaidi kuliko msimu uliopita.

Amewaomba mashabiki wa Yanga wampokee kwa mikono miwili na kumuunga mkono ili wamuongezee ari ya kuitumikia vizuri klabu hiyo kongwe nchini.

Ngasa alisema uamuzi wake wa kurejea Yanga umetokana na mapenzi yake mwenyewe na kusisitiza kuwa, ataendelea kuziheshimu Simba na Azam kwa sababu zimemsaidia kisoka na kimaisha.

No comments:

Post a Comment