KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, July 5, 2013

MARIAMU AWA KINYOZI BORA ARUSHA



NA SHAABAN MDOE, ARUSHA.
MSICHANA Mariamu Miraji (25), mkazi wa Arusha, ameibuka mshindi baada ya kuwabwaga wanaume 33 katika shindano la kumsaka kinyozi bora lililofanyika jana mjini hapa.
Shindano hilo liliwashirikisha vinyozi 35 kutoka saluni mbalimbali za mjini Arusha, akiwemo msichana mwingine, Janeth Kimaro.

Jaji mkuu wa shindano hilo, Koroli Mbise alisema Mariamu aliibuka mshindi kutokana na kufuzu vigezo mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kujieleza bila kusita katika kujibu maswali aliyoulizwa na jopo la majaji.

Alizitaja sifa zingine zilizomwezesha Mariamu kushinda shindano hilo kuwa ni kunyoa kwa wakati uliopangwa na ubora wa kazi yake kupitia mtindo wa 'Low cut' aliotakiwa kuutumia.

Kufuatia ushindi huo, Mariamu alizawadiwa televisheni ya ukubwa wa inchi 42 aina ya LG yenye thamani ya shilingi 1,600,000, mashine moja ya kunyolea pamoja na cheti cha kumtambulisha.

Mshindi wa pili wa shindano hilo alikuwa Abdul Razak, aliyejipatia zawadi ya simu ya mkononi aina ya Sony Ericson yenye thamani ya shilingi 100,000,mashine moja ya kunyolea pamoja na cheti.

Nafasi ya tatu ilinyakuliwa na Andrew Modest aliyezawadiwa simu ya mkononi aina ya Sony Ericson yenye thamani ya shilingi 80,000,mashine moja ya kunyolea pamoja na cheti. Washiriki wengine wa shindano hilo walizawadia vyeti vya ushiriki.

Akizungumza baada ya kutangazwa kwa washindi hao, Diwani wa Kata ya Kati, Abdul Tojo aliahidi kuwa, Jiji la Arusha pamoja na uongozi mzima wa serikali utayaendeleza mashindano hayo ili yatambulike kitaifa.

Abdul, ambaye alimwakilisha Meya wa Jiji la Arusha, alisema watamtangaza mshindi huyo mwanamke ili aweze kupata kazi nyingi za kimkoa kwa lengo la kuwapa ari wanawake wengine kujitokeza kufanya kazi hiyo badala ya kuiona kuwa ni ya wanaume pekee.

Mkurugenzi wa saluni ya Mnyampaa Baber Shop, iliyomtoa mshindi huyo, Charles Kisuke alisema, lengo lake ni kumtumia Mariamu katika kuitangaza kazi hiyo ya kunyoa kama kazi nyingine na kwa watu wote wakiwemo wanawake.

Charles alisema kwa sasa anajipanga zaidi kusambaza huduma zake hizo katika maeneo mbalimbali ya jiji la Arusha na mikoani ili kuhakikisha huduma za kinyozi zinapatikana kwa watu wote, hasa wageni wanaofika katika mkoa wa Arusha kwa shughuli mbalimbali.

Mratibu wa shindano hilo, Zuberi Mwinyi aliahidi kuliendeleza kwa kuliendesha kila mwaka kama njia ya kuitangaza kazi hiyo kitaifa na kuondoa dhana kwamba kazi hiyo ni kwa ajili ya watu wasio na kazi maalumu.

Alisema kwa mwaka ujao wa 2014, anatarajia kuboresha zaidi shindano hilo ikiwa ni pamoja na kuongeza zawadi na wigo wa washiriki

No comments:

Post a Comment