KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, July 3, 2013

SIMBA YAMNASA NYOTA WA SUDAN

BENCHI la ufundi la klabu ya Simba jana lilitarajiwa kuwafanyia majaribio wachezaji wapya wawili kutoka Uganda na Sudan Kusini.

Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hanspope aliwataja wachezaji hao kuwa ni Assumani Kayinzi, aliyekuwa akicheza soka ya kulipwa Vietnam na Kon James kutoka Al Nasri Juba ya Sudan Kusini.

Kayinzi alikuwa akicheza timu moja na mshambuliaji wa zamani wa Simba, Danny Mrwanda na beki Moses Oloya wa Uganda, ambaye alikuwa akiwindwa pia na klabu hiyo ya Msimbazi.

Kon ni mmoja wa wachezaji waliong'ara wakati Al Nasri ilipomenyana na Azam katika mechi ya michuano ya Kombe la Shirikisho na kutolewa kwa jumla ya mabao 8-1.

Hanspope alisema wachezaji hao wanakuja nchini kwa ajili ya majaribio na iwapo watamvutia Kocha Abdalla Kibadeni, watasajiliwa.

Mwenyekiti huyo wa kamati ya usajili ya Simba alimwelezea Kayinzi kuwa ni mchezaji mwenye uzoefu mkubwa na ambaye wana matumaini atakidhi vigezo vya Kibadeni.

Tayari Simba inao wachezaji watatu wa Uganda katika kikosi chake, kipa Abbel Dhaira, beki Samuel Ssenkoom na kiungo Mussa Mudde. Dhaira na Mudde wanaingia katika msimu wa pili Msimbazi wakati Ssenkoom utakuwa msimu wake wa kwanza.

Wakati huo huo, beki Shomari Kapombe wa Simba amechelewa kwenda Uholanzi kufanyiwa majaribio ya kucheza soka ya kulipwa kutokana na kukabiliwa na majukumu ya kuichezea Taifa Stars.

Kapombe alitakiwa kwenda Uholanzi tangu Juni 28 mwaka huu, lakini alishindwa kutokana na Taifa Stars kukabiliwa na mechi muhimu ya michuano ya awali ya Kombe la Dunia dhidi ya Ivory Coast.

Wakala wa mchezaji huyo, Denis Kadito alisema jana kuwa, kuchelewa kwa Kapombe kwenda kufanya majaribio hayo katika klabu ya FC Twente huenda kukavuruga mipango hiyo.

Hata hivyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hanspope alisema jana kuwa, Kapombe anatarajiwa kwenda Uholanzi baada ya Taifa Stars kumenyana na Uganda katika mechi ya michuano ya Kombe la CHAN.

No comments:

Post a Comment