KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, July 5, 2013

SJMC, TASWA KUENDESHA MAFUNZO KWA WAANDISHI WA HABARI ZA MICHEZO



SHULE Kuu ya Uandishi wa Habari na Mawasiliano kwa Umma (SJMC) ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kwa kushirikiana na Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA), wataendesha mafunzo ya siku tano kwa waandishi wa habari za michezo nchini.

Akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Makamu Mkuu wa SJMC, Dk. Michael Andindilile alisema mafunzo hayo yatafanyika Agosti mwaka huu na yataendeshwa na wahadhiri kutoka chuoni hapo, waandishi wa siku nyingi na wataalamu wa michezo mbalimbali.

“Tunao wahadhiri waliobobea katika tasnia ya habari, lakini pia wapo waandishi wa habari wakongwe ambao ni waalimu kitaaluma, pia tutachukua wataalamu wa michezo mbalimbali kuja kufundisha kwa siku hizo tano,” alisema Dk. Andindilile.

Makamu Mkuu huyo wa SJMC, aliupongeza uongozi wa TASWA kwa wazo lao la kushirikiana na SJMC na kuongeza kuwa, mafunzo hayo yatachukua siku tano na yatafanyika Dar es Salaam yakihusisha washiriki 45 kutoka vyombo mbalimbali vya habari katika tarehe itakayotangazwa.

Alisema wataalamu wa michezo mbalimbali kama vile soka, riadha, netiboli, gofu, kikapu, wavu na mikono watapata fursa ya kutoa mada kuhusiana na michezo yao na kwamba TASWA na SJMC wanashirikiana katika kuomba wadhamini wasaidie mafunzo hayo.

“Hii ni awamu ya kwanza kwa waandishi wachanga na baadhi ya wa kada ya kati, baada ya hapo tutaendesha mafunzo ya namna hii kwa waandishi wa siku nyingi wa habari za michezo na wahariri wa habari za michezo, tunaamini baada ya hapo kutakuwa na mabadiliko upande wa uandishi wa habari za michezo,” alisema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TASWA, Juma Pinto aliishukuru SJMC kwa kukubali kushirikiana na TASWA na kwamba siku zote chama chake kimekuwa kikipigania kuandaa mafunzo kwa wanahabari wa michezo kama sehemu mojawapo ya kukuza weledi.

“Fursa hii ni moja ya jitihada za TASWA kuhakikisha waandishi wa habari za michezo wanapata nafasi ya kujifunza zaidi kuhusu namna bora ya kuripoti habari za michezo kwa ujumla wake, hivyo nafasi hii si tu itasaidia wanachama wa TASWA bali pia na vyombo vya habari na washiriki hawatalipia chochote.

“Tunaamini waandishi wanapoboresha uandishi wao, inachangia kwa kiasi kikubwa kukuza heshima ya vombo vya habari, hivyo tunaomba wadau mbalimbali washirikiane nasi kudhamini mafunzo haya,” alisema Pinto na kuongeza kuwa kwa kushirikiana na SJMC wanaamini siku za usoni wanaweza kuandaaa mafunzo ya muda mrefu.

No comments:

Post a Comment