KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, July 14, 2013

TAIFA STARS YAKERA MASHABIKI

Taifa Stars imeshindwa kuutumia vizuri uwanja wa nyumbani baada ya leo (Julai 13 mwaka huu) kufungwa bao 1-0 na Uganda (The Cranes) katika mechi ya kwanza ya mchujo kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Wachezaji wa Ligi za Ndani (CHAN) zitakazofanyika mwakani nchini Afrika Kusini.


Denis Iguma ndiye aliyefunga bao hilo pekee kwa Uganda dakika moja baada ya mwamuzi Thierry Nkurunziza kutoka Burundi kupuliza filimbi kuanzisha kipindi cha pili cha mechi hiyo iliyochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Akizungumzia matokeo hayo, Kocha wa Stars, Kim Poulsen amesema mpira wa miguu ni mchezo wa kufunga mabao ambapo timu ilipata nafasi nzuri katika dakika ya kwanza tu lakini ilishindwa kuibadili kuwa bao.

“Uganda walitengeneza nafasi moja tu katika kipindi cha kwanza wakati sisi tulikuwa nazo kadhaa. Kipindi cha pili tuliwapa nafasi wakafunga bao lao. Lakini kwa kifupi kama wao wameweza kufunga hapa (Dar es Salaam), hata sisi tunaweza kufunga Kampala,” amesema Kim akizungumzia nafasi ya timu yake kusonga mbele.

Timu hizo zitarudiana jijini Kampala kati ya Julai 26 na 27 mwaka huu ambapo mshindi ndiye atakayepata tiketi ya kwenda kwenye fainali za tatu za CHAN zitakazofanyika Afrika Kusini. Stars ilicheza fainali za kwanza za CHAN zilizofanyika mwaka 2009 nchini Ivory Coast.

No comments:

Post a Comment