KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, July 3, 2013

SHAMBA LA BIBI KUKAMILIKA NOVEMBA

WAZIRI wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara amesema ukarabati unaoendelea kufanyika katika Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam utakamilika kabla ya Novemba mwaka huu.

Fenella alisema hayo jana alipozungumza na waandishi wa habari kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Alisema baada ya kukamilika kwa ukarabati, uwanja huo utaanza kutumika kwa ajili ya michuano mbalimbali.

Waziri Fenella alisema ukarabati wa uwanja huo umekuwa ukifanywa na kampuni moja ya China na kuongeza kuwa, kwa sasa upo kwenye hatua nzuri kabla ya kukamilika.

Katika hatua nyingine, Waziri Fenella amesema serikali inaendelea kutafuta mdhamini kwa ajili ya kuendesha Uwanja wa Taifa wa Dar es Salaam.

Waziri Fenella amesema lengo la kusaka mdhamini wa kuwekeza kwenye uwanja huo ni kuuongezea mapato na pia kutangaza vivutio vya kitalii nje ya nchi.

Dk. Fenella alisema hayo jana wakati alipokabidhiwa rasmi uwanja huo na Balozi wa China hapa nchini, Luyon Ring katika hafla iliyofanyika kwenye uwanja huo.

Alisema vivutio vya kitalii wanavyotarajia kuvitangaza kupitia uwanja huo ni pamoja na Mlima Kilimanjaro, mbuga za wanyama na madini.

Kwa kuanzia, Dk. Fenella alisema tayari wameshaanza kuutangaza uwanja huo kupitia matangazo mbalimbali ya moja kwa moja yanayoonyeshwa na kituo cha televisheni cha Superspot.

Alisema hawawezi kuendelea kutegemea mapato ya milangoni kwa ajili ya kuendesha uwanja huo kwa vile ni madogo na hayakidhi gharama za uendeshaji.

Alitoa mwito kwa mashabiki wa soka wanaofika kwenye uwanja huo kwa ajili ya kushuhudia mechi mbalimbali kuutunza na kuacha tabia ya kubomoa vitu na vifaa vingine muhimu.

Kwa upande wake, Balozi Luyon alisema anaamini watanzania watautunza uwanja huo ili kuenzi uhusiano mzuri uliopo kati ya serikali ya China na Tanzania.

Mhandisi wa kampuni ya Beijing, Nang alisema uwanja huo ni bora kati ya viwanja vilivyopo sasa barani Afrika kutokana na kuwa na kumbi nyingi za mikutano na ofisi.

Uwanja wa Taifa umejengwa na Kampuni ya Beijing Construction Engineering Group (T) Ltd (BCEG) ya China kwa gharama za dola milioni 56.4 za Marekani (sawa na sh. bilioni 80). Uwanja huo una uwezo wa kuchukua watazamaji 60,000.

No comments:

Post a Comment