KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, July 3, 2013

AFANDE SELE ATEMA CHECHE

MSANII nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini, Selemani Msindi 'Afande Sele' amesema, uamuzi wa serikali kutoza kodi kazi za wasanii ni mzuri, lakini hautakuwa na maana iwapo itashindwa kulinda kazi zao.

Akizungumza na Burudani mjini Morogoro wiki hii, Afande Sele alisema serikali inapaswa kutengeneza mazingira mazuri ya kulinda kazi za wasanii, ambazo bado zinaendelea kuuzwa holela nchini.

Afande Sele alisema kabla ya serikali kupitisha uamuzi huo, ilipaswa kukomesha kwanza wizi wa kazi za wasanii ili iweze kupata fedha nyingi za kodi na pia kuwakomboa wasanii kimapato.

Alisema ilivyo sasa ni sawa na mtu kupanga kulima shamba na kutarajia kupata mavuno mengi bila ya kuweka mazingira mazuri ya kuhakikisha kuwa, shamba lake linalindwa.

"Ni kweli serikali imeweka utaratibu huo kwa nia nzuri, lakini bado haijaweka mazingira mazuri ya kulinda kazi za wasanii,"alisema.

"Hadi leo hii CD za nyimbo za wasanii zinaendelea kutengenezwa na kuuzwa holela mitaani, nyimbo za wasanii zinatumika kama miito ya simu bila wenyewe kunufaika kwa lolote huku kazi zao zikiwa haziuziki,"aliongeza msanii huyo, ambaye aliwahi kutwaa taji la Mfalme wa Mashairi.

"Lazima serikali iwalinde wasanii kwa sababu ilivyo sasa, wanaonufaika bado ni wachache, wengi hawafaidiki kwa lolote,"alisisitiza.

Afande Sele alisema sheria zilizopo sasa za kulinda kazi za wasanii hazina nguvu na zinaendelea kutoa mwanya kwa baadhi ya wafanyabiashara wasio waaminifu kutumia kazi za wasanii kwa manufaa yao.

Alisema licha ya kuwepo kwa Chama cha Hatimiliki nchini (COSOTA), kimeshindwa kusimamia vyema majukumu yake kutokana na kuwa na watumishi wachache.

Msanii huyo pia alilitupia lawama Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) kwa kushindwa kuwasaidia wasanii, lakini alisema huenda ni kutokana na kutokuwa na nguvu ya kufanya hivyo.

"Leo hii ukipanda basi na kusafiri nalo kwenda mikoani, mwanzo wa safari hadi mwisho mtawekewa kanda za sinema za wasanii wa Bongo na kupigiwa nyimbo zao.

"Ukitembelea kumbi za burudani, utasikia nyimbo za wasanii wa Tanzania zikipigwa mwanzo wa onyesho hadi mwisho. Ukipita mitaani, kuna vibanda vinaonyesha filamu za Kitanzania na kutoza viingilio.

"Huwezi kuwalaumu wananchi hawa kwa sababu sio kosa lao. Ni kwa sababu hawajui sheria. Wahusika wanaosimamia sheria za hatimiliki wapo na wanaona, lakini wanashindwa kuchukua hatua. Kwa staili hii, hatuwezi kufanikiwa,"alisema msanii huyo mwenye kipaji cha kutunga nyimbo zenye mashairi yenye mvuto.

Afande Sele aliishauri serikali izifanyie marekebisho sheria mbovu na zilizopitwa na wakati zinazohusu wizi wa kazi za sanaa ili iweze kutekeleza vyema mpango wake wa kutoza kodi kazi za wasanii.

No comments:

Post a Comment