KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, July 11, 2013

NYOTA MPYA SIMBA KAMA OKWI



KLABU ya Simba imetamba kuwa, kusajiliwa kwa mshambuliaji mpya Amissi Tambwe kutoka Vital'O ya Burundi kutamaliza tatizo la ufungaji mabao katika timu hiyo msimu ujao wa ligi.

Tambwe ni mmoja wa washambuliaji nyota wa Vital'O, ambayo ilitwaa ubingwa wa michuano ya Kombe la Kagame iliyomalizika hivi karibuni katika jimbo la Darfur nchini Sudan. Katika michuano hiyo, Tambwe aliibuka mfungaji bora kwa kufunga mabao sita.

Uwezo wa mshambuliaji huyo katika kuwatoka mabeki wa timu pinzani na kufunga mabao, umefananishwa na ule aliokuwa nao mshambuliaji wa zamani wa Simba, Emmanuel Okwi, ambaye aliuzwa kwa klabu ya Etoile du Sahel ya Tunisia.

Mwenyekiti wa kamati ya usajili ya Simba, Zacharia Hanspope alisema kwa njia ya simu jana akiwa nje ya nchi kuwa, Tambwe ameshawasili nchini kwa ajili ya kufanya mazungumzo na uongozi wa Simba.

"Kwa sasa nipo nje ya nchi kikazi, natarajia kurudi Tanzania leo au kesho, lakini tayari nimeshafanya mazungumzo ya awali na Tambwe na kimsingi tumekubaliana mambo mbalimbali. Kinachosubiriwa ni kumfanyia majaribio mchezaji huyo,"alisema Hanspope.

Mwenyekiti huyo wa kamati ya usajili ya Simba alisema, kwa mujibu wa utaratibu waliouanzisha, hakuna mchezaji atakayesajiliwa bila kufanyiwa majaribio na benchi la ufundi, linaloongozwa na Kocha Abdalla Kibadeni.

"Iwapo benchi la ufundi litampitisha, uongozi utampatia mkataba wa miaka miwili wa kuichezea Simba kuanzia msimu ujao. Hatutaki kununua Mbuzi kwenye gunia na pia tupo makini kumlinda kwa sababu tumesikia wenzetu wameshaanza kumvizia,"alisema.

Tambwe alitua nchini juzi na anamsubiri Hanspope ili wamalize mazungumzo yao kabla ya kufanyiwa majaribio na kumwaga wino Simba. Ligi Kuu ya Tanzania Bara imepangwa kuanza Agosti 24 mwaka huu.

Wachezaji wengine wapya kutoka nje, ambao wamekuwa wakifanyiwa majaribio na Simba ni Assumani Kayinzi, aliyekuwa akicheza soka ya kulipwa Vietnam na Kon James kutoka Al Nasri Juba ya Sudan Kusini.

Wachezaji pekee wa kigeni waliosajiliwa Simba hadi sasa ni kipa Abel Dhaira, beki Mussa Mudde na Samuel Ssenkoom, ambaye msimu ujao utakuwa wa kwanza kwake kuichezea Simba. Dhaira na Mudde wapo Simba tangu msimu uliopita.

Kwa mujibu wa kanuni za usajili, kila klabu inayoshiriki michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara inatakiwa kusajili wachezaji watano wa kigeni.

No comments:

Post a Comment