KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, July 11, 2013

WABOGOJO SASA ANAPIGA SHOO ZA KIMATAIFA MACAU



Je, unamkumbuka msanii Athumani Ford, aliyekuwa maarufu kwa jina la Wabogojo? Yule aliyekuwa akipamba video za nyimbo za msanii nyota wa muziki wa kizazi kipya, Lucas Nkenda 'Mr Nice'?
Sifa moja kubwa aliyokuwa nayo Wabogojo wakati huo hapa nchini ni kuvichezesha viungo vya mwili wake anavyotaka. Vitendo vyake, ambavyo havikuwa na tofauti na mchezo wa sarakasi, vilimfanya aonekane mtu wa ajabu.
Watanzania wengi walianza kumuona na kumfahamu Wabogojo wakati aliposhiriki kuipamba video ya wimbo wa Kikulacho ya Mr. Nice. Alikuwa anafurahisha kutokana na vitendo vyake.
Ni baada ya kuonekana kwenye video hiyo, Wabogojo akaanza kujulikana ndani na nje ya nchi. Wajanja wakabaini kwamba, mchezo anaoucheza ni 'dili'. Wakampa shavu.
Hivi sasa Wabogojo yupo kwenye kisiwa cha Macau kilichopo China, akifanya maonyesho kwenye kumbi mbalimbali za burudani. Inaaminika kuwa, kisiwa hiki kinakaliwa na watu wenye uwezo mkubwa kipesa.
Wabogojo ameandika kupitia kwenye mtandao wake hivi karibuni kuwa, alipata ulaji huo baada ya kufanya ziara ndefu barani Ulaya akiwa na kundi la Mother Africa.
"Kwa ufupi, baada ya ziara ya Ulaya tukiwa na kundi la Mama Africa, ambako tulipelekwa na Winston Ruddle, tukafanikiwa kupata kazi nyingine na ndio hii ya sasa,"alisema msanii huyo.
Wabogojo alisema mazoezi ya maonyesho wanayoyafanya sasa huko Macau, waliyafanya kuanzia Februari 2009 hadi Machi 2012 katika kituo cha michezo cha Antwerpen kilichopo Ubelgiji.
"Baada ya mazoezi hayo, tukaja Macau na kuandaa maonyesho. Tulianza maonyesho yetu kuanzia Septemba 17, 2012 na mkataba ni mzuri. Tumalipwa pesa nzuri kwa mwezi hadi raha!!" Ameeleza msanii huyo.
Kwa mujibu wa Wabogojo, wataendelea kuwepo Macau hadi Septemba 2014. Alisema uwepo wao zaidi kwenye kisiwa hicho utategemea mkataba mpya.
Hata hivyo, Wabogojo alisema msanii yupo huru kukatisha mkataba wake iwapo ataona amechoshwa na kazi hiyo.
Katika kikundi chao, Wabogojo alisema wapo wasanii 12 kutoka Tanzania. Alisema wengine wanatoka katika nchi za Brazil, Uingereza na Marekani.
Akifafanua kuhusu kisiwa cha Macau, Wabogojo alisema watu wenye uwezo wa kifedha kutoka sehemu mbalimbali duniani, hupenda kwenda kufanya matanuzi huko.
"Ni kisiwa chenye makasino mengi. Watu huja kutumia pesa zao tuu. Ni kama kulivyo Las Vegas kule Marekani,"alisema.
Alisema maonyesho ya kundi lao yanayojulikana kwa jina la The House of Dancing Water, yanafanyika kwenye kasino kubwa zaidi inayojulikana kwa jina la City of Dream.
" Tumejifunza mambo mengi tangu tulipofika huku. Tumejifunza kuogelea na kupiga mbizi baharini na kwenye mabwawa ya kuogelea. Kama hujui kuogelea, maonyesho haya hayakufai,"alisema.
Wabogojo alisema anamshukuru Mr. Nice kwa kumtambulisha kwenye ulimwengu wa sanaa, japokuwa hakuwa akimlipa vizuri kutokana na kazi yake hiyo. Anasema alichokipata ni zaidi ya pesa.
"Mungu yu mwema," alimalizia maelezo yake kupitia kwenye mtandao huo.
Wabogojo ni kama yake prodyuza maarufu wa muziki wa kizazi kipya nchini, Razakl Ford wa Kampuni ya 4D Videos, aliyetengeneza video ya wimbo wa Recho, unaojulikana kwa jina la Upepo. Pia ni kaka wa mwigizaji nyota wa filamu za kibongo, Shamsa Ford.

No comments:

Post a Comment