KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, January 9, 2012

Azam yazua balaa Yanga

HALI si shwari kwa klabu ya Yanga baada ya baadhi ya wachezaji nyota wa timu hiyo kutishia kugoma kwa madai ya kupinga kulipwa nusu ya mishahara yao.
Tishio la wachezaji hao limekuja siku moja baada ya timu hiyo kuchapwa mabao 3-0 na Azam katika mechi ya michuano ya Kombe la Mapinduzi iliyochezwa juzi kwenye Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
Kipigo ilichokipata Yanga kimeifanya ifungashe virago katika michuano hiyo na timu hiyo ilitarajiwa kurejea Dar es Salaam jana jioni kwa boti ikitokea Zanzibar.
Wakizungumza na Mzalendo kwa njia ya simu kutoka Zanzibar jana, baadhi ya wachezaji hao walisema uamuzi wa uongozi kuwalipa nusu ya mshahara kila mchezaji haukuwafurahisha.
Wachezaji hao, ambao hawakutaka majina yao yatajwe gazetini walisema, kabla ya kwenda Zanzibar, walikutana na kujadiliana kuhusu uamuzi wa uongozi kuwalipa mishahara nusu.
Mmoja wa wachezaji hao alisema, kitendo hicho kiliwafanya wagawanyike, ambapo wengine walikubali kwenda Zanzibar kushiriki mashindano hayo huku wengine wakigoma.
Hata hivyo, mchezaji huyo alisema baada ya mvutano mkali kati yao, walikubali kwenda Zanzibar, lakini walitaka wakutane na uongozi ili kujadili tatizo hilo.
Kufuatia uongozi kushindwa kueleza hatma yao, mchezaji mwingine alisema, wamepanga kugoma kufanya mazoezi hadi watakapomaliziwa mishahara yao.
“Huo ndio msimamo tuliofikia kwa sababu hali kwa kweli ni mbaya sana, kila mchezaji ana matatizo na viongozi wetu hawatujali. Hatuelewi tutaishi vipi,”alisema mmoja wa wachezaji waandamizi wa klabu hiyo.
Tishio la mgomo la wachezaji hao limekuja siku chache baada ya Kocha Mkuu wa timu hiyo, Kostadin Papic kupasua jipu, akieleza kuwa, wachezaji na benchi la ufundi hawajalipwa mishahara kwa miezi miwili.
Alipoulizwa kuhusu tishio hilo la wachezaji jana, Ofisa Habari wa Yanga, Louis Sendeu alisema hana taarifa yoyote.
Sendeu alisema anachofahamu ni kwamba, timu ilitarajiwa kurejea Dar es Salaam jana jioni na kuingia moja kwa moja kambini kujiandaa kwa mechi yao ya awali ya michuano ya klabu bingwa Afrika dhidi ya Zamalek ya Misri.
Akizungumzia kipigo cha juzi kutoka kwa Azam, Sendeu alisema ni matokeo ya kawaida ya mchezo na kwamba hakiwezi kusababisha timu yao isambaratike.
Katika mechi ya juzi, Azam ilijipatia mabao yake kupitia kwa John Boko na Kipre Tchetche, aliyefunga mabao mawili.
Wakati huo huo, Mafunzo juzi ilifuzu kucheza nusu fainali ya michuano hiyo baada ya kuichapa Kikwajuni bao 1-0 katika mechi iliyochezwa jioni kwenye uwanja huo.
Bao pekee na la ushindi la Mafunzo lilipachikwa wavuni na mshambuliaji Sadik Habib dakika ya 59.

No comments:

Post a Comment