KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, January 5, 2015

AZAM YAICHAPA KMKM 1-0


Mabingwa wa Tanzania Bara, Azam FC wamepata ushindi wa kwanza katika Kombe la Mapinduzi, baada ya kuwalaza mabingwa wa Ligi Kuu visiwani hapa, KMKM 1-0 Uwanja wa Amaan, Zanzibar usiku huu.


Sifa zimuendee beki Shomary Kapombe aliyesababisha bao hilo pekee dakika ya 18, na kuifanya Azam FC sasa ifikishe pointi nne baada ya awali kutoa sare ya 2-2 na mabingwa watetezi, KCCA ya Uganda.

Bao hilo lililfungwa na Khamis Ali ‘Chichi’, Nahodha wa KMKM aliyejifunga kwa kichwa akijaribu kuokoa shuti la Shomary Kapombe alilopiga kutoka umbali wa mita 25.

Mchezo ulikuwa mkali na timu hizo zilishambuliana kwa zamu muda wote, huku KMKM wakipoteza nafasi nyingi za kufunga kipindi cha pili.

KCCA sasa inaongoza Kundi B kwa pointi zake nne, sawa na Azam FC, lakini yenyewe ina wastani mzuri wa mabao baada ya jioni ya leo kuifunga Mtende mabao 3-0.

Mechi nyingine zilizochezwa leo, Taifa ya Jang’ombe imeilaza 1-0 Shaba Uwanja wa Mao dze Tung, wakati Yanga SC imeifunga Polisi mabao 4-0, mechi zote za Kundi A.

Michuano hiyo, itaendelea kesho kwa mechi za mwisho za Kundi C, Mtibwa Sugar wakimenyana na Mafunzo Saa 10:00 jioni na baadaye Simba SC na JKU Saa 2:15 usiku Uwanja wa Amaan, Zanzibar.

Azam FC; Mwadini Ali, Shomary Kapombe, Gardiel Michael, David Mwantika, Aggrey Morris, Mudathir Yahya, Erasto Nyoni, Salum Abubakar, John Bocco, Amri Kiemba na Brian Majwega.

KMKM; Mudathir Khamis, Abdulkadir Nemihi, Mwinyi Hajji Mngwali, Ibrahim Khamis Khatib, Khamis Ali Khamis, Iddi Mbegu Mrisho, Nassor Ali Omar, Tizo Chombo, Fakhi Mwalimu, Halid Hebi na Maulid Ibrahim Kapenta.

No comments:

Post a Comment