KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, April 17, 2013

D0GO JANJA: SIKUFELI MITIHANI SABABU YA KUENDEKEZA STAREHE



MSANII machachari wa muziki wa kizazi kipya nchini, Abubakar Chende 'Dogo Janja' amesema si kweli kwamba amefeli mitihani ya kidato cha nne kutokana na kuendekeza starehe.

Akizungumza mjini Dar es Salaam wiki hii Dogo Janja alisema, kufeli kwake kulitokana na bahati mbaya na ni mambo ya kawaida katika mitihani kwa wanafunzi.

Dogo Janja alisema madai yaliyotolewa hivi karibuni na kiongozi wake wa zamani wa kundi la Tip Top Connections, Hamad Ally 'Madee' kwamba amefeli kutokana na kuendekeza sana starehe, yamelenga kumchafua.

"Nashangaa sana kwa nini Madee anaendelea kunifuatafuata. Wakati nikiwa Afrika Kusini, nilipigiwa simu na mtangazaji mmoja wa redio akiniambia kwamba, Madee ameniponda kwa kusema nimefeli tena kwa sababu ya kuendekekeza starehe.

"Madai haya hayana ukweli wowote. Mimi na yeye tulishamaliza tofauti zetu na kuamua kusameheana. Namheshimu kama mtu aliyenitoa na kunifikisha hapa nilipo, lakini sipendi tabia yake ya kunifuatafuata,"alisema.

Ofisa Taaluma katika shule ya sekondari ya Makongo, Alfred Mbaula alikaririwa akisema kuwa, mahudhurio ya Dogo Janja darasani yalikuwa mazuri na alikuwa akishirikiana vyema na wenzake.

Mbaula alisema Dogo Janja alifeli mitihani yake kwa wastani mdogo, ambao usingemruhusu kuendelea na kidato cha tatu, hivyo atalazimika kurudia kidato cha pili.

Alipoulizwa iwapo uongozi wa shule ulikuwa na taarifa ya safari ya Dongo Janja nchini Afrika Kusini, ofisa huyo alisema hakuwa ameomba ruhusa.

"Sio kweli kwamba aliomba ruhua na wala ofisi haina taarifa, japokuwa shule haina tatizo, akitoa taarifa hata katikati ya masomo iwapo anatakiwa kufanya shughuli za muziki kwa sababu Makongo ni shule ya vipaji,"alisema.

No comments:

Post a Comment