KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, January 16, 2013

OKWI KUIAGA SIMBA JAN 26

KLABU ya Simba imesema mshambuliaji wake, Emmanuel Okwi atawaaga mashabiki wa klabu hiyo katika mchezo wa kirafiki dhidi ya African Lyon utakaofanyika Januari 26, mwaka huu.

Katibu Mkuu wa Simba, Evodius Mtawala alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, Okwi ameamua kuwaaga mashabiki wa timu hiyo kutokana na kumpa ushirikiano mkubwa.

Hata hivyo, Mtawala alisema watalazimika kuomba ruhusa ya kumtumia mchezaji huyo kutoka katika klabu yake ya sasa ya Etoile Du Sahel ya Tunisia.

Simba imemuuza Okwi kwa Etoile Du Sahel kwa kitita cha dola 300,000 za Marekani (sawa na sh. milioni 480,000) baada ya kufuzu majaribio aliyofanyiwa.

Kwa mujibu wa Mtawala, kikosi cha Simba, ambacho kwa sasa kipo kambini nchini Oman, kinatarajiwa kurejea nchini Januari 23 mwaka huu kwa ajili ya maandalizi ya mwisho ya hatua ya pili ya ligi kuu ya Tanzania Bara.

Okwi ametia saini mkataba wa kuichezea Etoile Du Sahel kwa miaka miwili, ambapo atakuwa akilipwa mshahara wa dola 200,000 kwa mwaka. Pia amepewa nyumba ya kuishi na gari.

Mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Uganda, alijiunga na Simba miaka mitatu iliyopita akitokea SC Villa ya Uganda na kuiwezesha kufanya vizuri katika michuano ya ligi na kimataifa.

Wakati huo huo, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hanspope amesema hawana haraka ya kutafuta mchezaji wa kuziba nafasi ya Okwi.

Hanspope alisema jana kuwa, watalazimika kufanyakazi hiyo kwa umakini mkubwa ili waweze kumpata mchezaji mwenye kiwango kinachoshabihiana na Okwi.

Okwi amekuwa mchezaji wa tatu wa Simba kuuzwa nje kwa bei mbaya. Awali, Simba iliwauza mshambuliaji Mbwana Samatta na kiungo Patrick Ochan wa Uganda kwa klabu ya TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo kwa kitita cha dola 200,000.

No comments:

Post a Comment