KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, August 26, 2012

WACHEZAJI 11 KUTOKA NJE WAPATA ITC

Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea Hati ya Uhamisho wa Kimataifa (ITC) kwa wachezaji 11 wa nje kati ya 14 walioombea usajili na klabu mbalimbali za Ligi Kuu.

Wachezaji walioombewa usajili Yanga na tayari ITC zao zimepatikana ni Nizar Khalfan kutoka Vancouver Whitecaps ya Canada, Didier Kavumbagu (Atletico Olympic- Burundi) na Mbuyu Twite kutoka FC Lupopo ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC).

Kwa upande wa Simba ni Musa Mude (Sofapaka, Kenya) na Daniel Akuffor (Stella Abidjan, Ivory Coast) wakati Mtibwa Sugar ni Shabani Kisiga timu ya El Itihad ya Oman.

Waliopata ITC kwa upande wa Kagera Sugar ni Wilfred Ojodale Ame na Benjamin Efe Ofuyah wote kutoka FC Abuja ya Nigeria.

Wengine ni Deangelis Silva kutoka New Road ya Nepal kwenda Coastal Union, George Odhiambo kutoka Randers FC ya Denmark kwenda Mtibwa Sugar na Jerry Santo kutoka Tusker, Kenya kwenda Coastal Union.

Wachezaji ambao wameombewa usajili na ITC zao bado hazijapatikana ni Salum Kinje na Pascal Ochieng wa AFC Leopards, Kenya kwenda Simba na Ayoub Hassan Isiko kutoka Bull FC, Uganda kwenda Mtibwa Sugar.

Bado klabu ambazo hazijakamilisha usajili na kupata ITC zina fursa ya kufanya hivyo hadi Septemba 4 mwaka huu ambapo dirisha litafungwa.

Pia TFF imetoa ITC kwa wachezaji wanane walioombewa kwenda kucheza mpira wa miguu katika nchi za Kenya na Msumbiji kutoka katika klabu mbalimbali za hapa nchini. Wachezaji hao na klabu wanazokwenda katika mabano ni Abdallah Ally Abdallah (CD Madchegde, Msumbiji), Almasi Khatib Mkinda (Ferroviario da Beira, Msumbiji), David Naftali (Bandari, Kenya) na Hassan Hassan Mustafa (CD Madchegde, Msumbiji).

Wengine ni Meshack Abel (Bandari, Mombasa), Mohamed Banka (Bandari, Kenya), Thobias Davis Silas (CD Madchegde, Msumbiji) na Thomas Maurice (Bandari, Kenya).

VIPIMO VYA TIBA KWA WACHEZAJI

Klabu zote zilizowasilisha Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) maombi ya usajili kwa wachezaji wao zinatakiwa pia kuwasilisha nakala za hati zao za vipimo vya afya (medical certificate) kwa mujibu wa kanuni za usajili.

No comments:

Post a Comment