KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Tuesday, December 11, 2012

TASWA YASHANGAZWA NA WANACHAMA WAKE



CHAMA cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA) kinaendelea na maandalizi kwa ajili ya Mkutano Mkuu wa chama hicho utakaofanyika Desemba 21 na 22 mwaka huu Kiromo View Resort Hotel, Bagamoyo mkoani Pwani.
Kama tulivyosema wiki iliyopita kuwa mkutano huo unatarajiwa kushirikisha wanachama zaidi ya 100, ambao kushiriki kwao itabidi wathibitishe kwa njia ya maandishi kwa maana ya email ili uwepo wao uweze kuthaminika.
Lakini bado kuna mwitikio mdogo wa wanachama wanaothibitisha ushiriki wao, ambapo hadi kufikia leo saa tano asubuhi waliothibitisha ni 22 tu, hivyo tunasisitiza wengine wafanye hivyo haraka na tusikubali kufanya mambo kwa mazoea na mwisho wa kuthibitisha ni Jumamosi Desemba 15, saa kumi alasiri na watakaokwama kufanya hivyo watahesabika wamekosa sifa ya kushiriki mkutano.
Tunaomba wanachama wote ambao wanatarajia kuhudhuria mkutano huo wathibitishe ushiriki wao kwa Katibu Mkuu wa TASWA kwa njia ya email: mgosius@yahoo.com au taswatz@yahoo.com.
Kamati ya Utendaji ya TASWA inaendelea na juhudi za kutafuta wadhamini kwa ajili ya Mkutano Mkuu, ambapo kiasi cha Sh. Milioni 20 kinahitajika kufanikisha mkutano ikiwa ni gharama mbalimbali ikiwemo chakula, malazi, usafiri kwa wanachama wa Dar es Salaam, pamoja na usafiri na malazi kwa wanachama wanaotoka nje ya Dar es Salaam.
Tayari wadau watatu wamejitokeza kupiga jeki mkutano huo, ambapo Alhamisi Desemba 13 saa tano asubuhi mgahawa wa City Sports Lounge Mwenyekiti wa TASWA, Juma Pinto atatangaza mdhamini mmoja ambaye tutakuwa tumemalizana naye.
Kiasi cha fedha kinachohitajika ni kikubwa sana, hivyo bado jitihada zinaendelea kutafuta wadhamini wengine kuhakikisha mkutano unakuwa wa mafanikio makubwa na tunaomba wenye nia ya kushirikiana nasi wafanye hivyo.
Licha ya wanachama pia tunatarajia katika mkutano huo pia watakuwepo wadau mbalimbali wa TASWA wakiwemo waandishi wakongwe wa habari za michezo ambao watapewa nafasi ya kuzungumza.
Wanachama wa TASWA watapata fursa ya kupokea na kujadili Ripoti ya Utendaji ya chama, Mapato na Matumizi, maendeleo ya chama na masuala mbalimbali yanayohusu waandishi wa habari za michezo kwa ujumla.
Pia kutakuwa na semina maalum itakayoendeshwa kwa washiriki wa mkutano huo ili wawe na uelewa kuhusiana na ajenda ya kuinua kipato kwa wanachama ambayo itajadiliwa kwenye mkutano huo.
Kamati ya Utendaji ya TASWA imekubaliana iwasaidie wanachama wake waweze kujitegemea kwa kuanzisha Chama cha Akiba na Mikopo (SACCO’S), lakini imeamua kwanza iwaite wataalamu wa vyama vya ushirika watoe elimu juu ya jambo hilo na kukishakuwa na uelewa wa kutosha suala hilo lipelekwe kama ajenda kamili ya kuanzisha chama hicho kwenye Mkutano Mkuu.

No comments:

Post a Comment