KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Saturday, December 1, 2012

PAPIC AISHIKA YANGA PABAYA, FIFA YATAKA MAELEZO



Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) limeitaka klabu ya Yanga kuwasilisha maelezo ya ziada na vielelezo kuthibitisha hoja zao dhidi ya mwalimu wa zamani wa klabu hiyo, Kostadin Papic ambaye ameishtaki klabu hiyo akidai malimbikizo ya mshahara yanayofikia Dola 12,000 za Kimarekani ifikapo Desemba 11, 2012.

Yanga, ambayo ilimuondoa kocha huyo Mserbia mwishoni mwa msimu wa mwaka 2011/12, inadai kuwa ilishafanya malipo kadhaa, yakiwemo ziada ya gharama za hoteli aliyokuwa akiishi, na kwamba hadi sasa kocha huyo anadai si zaidi ya Dola 4,000 za Kimarekani ambazo klabu hiyo imesema itamlipa mara atakapowasilisha ripoti ya ufundi ya kipindi alichokuwa kocha mkuu.

Katika barua yake kwa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), FIFA imeitaka Yanga kuwasilisha vielelezo hivyo kabla ya Desemba 11, 2012 baada ya Papic kuliandikia Shirikisho hilo akidai kuwa “haamini kwamba klabu hiyo itatekeleza ahadi yake ya kulipa deni walilolikubali” na kutaka kujua itachukua muda gani kulipa baada ya mtaalamu huyo kutoka Serbia kuwasilisha ripoti yake ya kiufundi kama alivyotakiwa na uongozi wa Yanga.

Katika barua hiyo ambayo imetakiwa iwasilishwe kwenye uongozi wa Yanga, FIFA imeeleza kuwa kama Yanga haitawasilisha hoja zaidi na vielelezo ifikapo tarehe hiyo, Shirikisho hilo litachukulia kuwa klabu haina haja ya kuwasilisha hoja zaidi na hivyo kuendelea na taratibu za kuliwasilisha suala hilo kwenye Kamati ya Hadhi za Wachezaji kwa ajili ya hatua zaidi na uamuzi ufanywe kwa mujibu wa nyaraka zilizopo.

Akizungumzia suala hilo, katibu mkuu wa TFF, Angetilke Osiah alisema barua hiyo ya FIFA itawasilishwa mapema Yanga ili iweze kujua hatua za kuchukua kuondoa uwezekanbo wa klabu hiyo kuchukuliwa hatua ambazo zinaweza kuzuilika.

Yanga pia ilikuwa kwenye hatari ya kushushwa daraja baada ya kushindwa kuwasilisha vielelezo mapema katika sakata lililomuhusu mchezaji wake wa zamani, John Njoroge ambaye aliishtaki klabu hiyo FIFA akidai fidia ya takmriban Sh milioni 17 kutokana na Yanga kuvunja mkataba wake bila ya kufuata taratibu.

Baada ya kuwasilisha mashtaka yake FIFA, Yanga iliandikiwa barua iwasilishe utetezi wake lakini ikashindwa kufanya hivyo na kesi hiyo kusikilizwa upande mmoja na Kitengo cha Usuluhishi cha FIFA (DRC) na kutoa uamuzi ambao ulimnufaisha beki huyo wa Kenya.

Katikati ya mwaka, FIFA ilitoa agizo la kukazia hukumu hiyo ikitoa siku 30 kwa Yanga kumlipa Njoroge na kwamba ingeshindwa kufanya hivyo suala hilo lingewasilishwa Kamati ya Nidhamu kwa ajili ya kuchukua hatua.

Katika barua yake, FIFA ilitaja baadhi ya hatua hizo kuwa ni kupokonywa pointi, kushushwa daraja au kulipishwa faini kubwa.

No comments:

Post a Comment