KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, December 13, 2012

KIPA WA KIMATAIFA WA UGANDA AMWAGA WINO SIMBA


Kipa mpya wa Simba, Abbel Dhaira (kulia) akipeana mkono na Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hanspope mara baada ya kutia saini mkataba wa kuichezea timu hiyo kwa miaka miwili leo.

Na Mahmoud Zubeiry

KIPA namba moja wa Uganda, Abbel Dhaira mbali na kusaini mkataba wa miaka miwili wenye thamani ya dola za Kimarekani 40,000, pia atakuwa akipokea mshahara wa Sh. Mlioni 2 kwa mwezi.

Dhaira alisaini mkataba jana katika hoteli ya JB Belmonte, Dar es Salaam mbele ya Katibu wa Simba, Evodius Mtawala na Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya klabu hiyo, Zacharia Hans Poppe.

Akizungumza na BIN ZUBEIRY jana, baada ya kumsajili kipa huyo, Hans Poppe alisema kwamba huyu ni kipa wa kwanza mwenye umbo kubwa tangu, kumalizika kwa zama za Mwameja Mohamed katika klabu hiyo.

“Naamini tumepata mtu sahihi na katika wakati mwafaka, hakuna asiyejua umahiri wa Dhaira langoni, sasa tunasubiri kuvuna matunda ya kumsajili,”alisema Hans Poppe, Kapteni wa zamani wa Jeshi la Wananchi Tanzania(JWTZ), ambaye leo anapanda ndege kwenda Uingereza kwa mapumziko ya Krisimasi na mwaka mpya.

Hans Poppe aliyepigana vita dhidi ya Uganda, alisema kwamba Dhaira ni kipa ambaye amependekezwa na kipa wao wa kwanza hivi sasa, Juma Kaseja hivyo anaamini wawili hao wataishi vizuri na kushirikiana.

Kwa upande wake, Dhaira ambaye anarejea leo kwao Uganda kwenda kuchukua vifaa vyake vya kazi kwa ajili ya kuja kuanza kumtumikia mwajiri wake mpya, alisema kwamba amefurahi kusaini Simba SC na atafanya vizuri ili kuwafurahisha mashabiki wa klabu hiyo.

“Simba ni klabu kubwa Afrika na inacheza Ligi ya Mabingwa Afrika, kuna wachezaji rafiki zangu na ndugu zangu, Mussa Mudde na Emmanuel Okwi, lakini Afrika Mashariki ni moja, wachezaji wote wa Simba ni ndugu zangu, nitajisikia nipo nyumbani kabisa”alisema Dhaira, anayetua Simba akitokea I.B.V FC ya Iceland.

Dhaira aliyeibukia Express ya Uganda mwaka 2006, mwaka 2008 alihamia U.R.A. pia ya Uganda, ambayo aliichezea hadi mwaka 2010 alipohamia Ulaya.

Kwa kumpata Dhaira, Simba SC imepata kipa wa uhakika wa kusaidiana na kipa wake wa kwanza, Juma Kaseja ambaye amekuwa akisoteshwa peke yake bila kupumzika.

(Habari, picha kwa hisani ya blogu ya Bin Zubeiry)

No comments:

Post a Comment