KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, December 7, 2012

KAMATI YA MGONGOLWA KUJADILI SAKATA LA NGASA



Sekretarieti ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imemwandikia mwenyekiti wa Kamati ya Sheria, Katiba na Hadhi za Wachezaji kumuomba kuitisha kikao cha dharura kuzungumzia shauri la mshambuliaji wa Azam, Mrisho Khalfan Ngassa ambaye kwa sasa anaichezea klabu ya Simba kwa mkopo.
Mshambuliaji huyo hatari wa kimataifa amezua tafrani baina ya klabu hizo mbili baada ya kuomba uhamisho kwenda klabu ya El Mereikh ya Sudan ambayo imeweka dau kubwa la kumnunua baada ya kung’ara kwenye michuano ya Kombe la Chalenji mjini Kampala.
Kutokana na maombi hayo, Azam imeiandikia Simba ikiitaarifu kuwa inataka kumrejesha mchezaji huyo na kwamba iko tayari kurejesha kiasi cha Sh milioni 25 ambazo Simba iliilipa Azam ili imruhusu mshambuliaji huyo wa zamani wa Yanga kuichezea klabu hiyo ya Mtaa wa Msimbazi kwa mkopo hadi Mei mwakani.
Hata hivyo, Simba inadai kuwa ina haki ya kushirikishwa katika suala lolote linalohusu kuuzwa kwa mchezaji huyo kwa kuwa katika mkataba wa kumchukua mchezaji huyo wa mkopo pande hizo mbili zilikubaliana kuwa haki zote zilozo kwenye mkataba wake na Azam zilipwe na Simba.
Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah alisema kuwa amemuomba mwenyekiti wa Kamati hiyo ya TFF kuitisha kikao mapema ili suala hilo lipatiwe ufumbuzi mapema na kuondoa hali ya kutoelewana baina ya wawakilishi hao wa Tanzania kwenye michuano ya klabu ya Afrika mwakani.
Angetile alisema TFF imepokea barua nne kutoka klabu za Simba na Azam zinazozungumzia kuuzwa kwa mchezaji huyo mbili kutoka Azam zikitaarifu kuwa zinamrejesha Ngassa kwenye klabu hiyo na kueleza nia ya kumuuza kwenda El Merreikh na nyingine mbili za Simba zikipinga uuzwaji huo na kuiomba TFF isitoe Cheti cha Uhamisho wa Kimataifa (ITC) hadi hapo suala hilo litakapopatiwa ufumbuzi.
Ngassa alichukuliwa na Simba mara baada ya michuano ya Kombe la Kagame katika uhamisho ambao haukutegemewa na wengi wakati Azam ilipomuweka sokono kwa mkopo, ikiwa ni siku chache baada ya nyiota huyo kufunga bao na kwenda upande wanaokaa mashabiki wa Yanga kuibusu jezi ya klabu hiyo ya Mtaa wa Jangwani na baada ya mechi kutokea mlango ulio chini ya jukwaa wanalokaa mashambiki wa Yanga.
Kitendo hicho kilitafsiriwa kuwa alikuwa akionyesha mapenzi makubwa na klabu hiyo aliyoichezea akitokea Kagera Sugar katika kipindi ambacho mchezaji huyo alikaririwa waziwazi akiwalaumu viongozi wa Azam kuwa wanamtuhumu kucheza chini ya kiwango kila timu yake inapokutana na Yanga

No comments:

Post a Comment