KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, June 7, 2012

NSAJIGWA: Sina mpango wa kustaafu soka






Asema hajutii kutemwa Taifa Stars

Alilia NSSF kwa wanasoka wa Bongo

NAHODHA wa zamani wa timu ya soka ya Taifa, Taifa Stars, Shadrack Nsajigwa amesema hana mpango wa kustaafu mchezo huo licha ya kuwepo kwa tetesi kwamba ataachwa kwenye kikosi cha Yanga kwa ajili ya msimu ujao wa ligi. Katika makala hii ya ana kwa ana iliyoandikwa na Mwandishi Wetu, ATHANAS KAZIGE, beki huyo anaelezea kuhusu msimamo wake huo na masuala mengine mbalimbali.

SWALI: Kuna habari zilizozagaa kwenye vyombo vya habari na mitandao mbalimbali kwamba umepanga kustaafu kucheza soka baada ya msimu huu kumalizika. Je, kuna ukweli wowote kuhusu habari hizi?
JIBU: Nisingependa kujibu swali hilo kwa wakati huu, lakini kama kungekuwa na ukweli wowote, lazima ningekueleza ndugu yangu.
SWALI: Umeupokeaje uamuzi wa Kocha Kim Poulsen kukuacha kwenye kikosi cha Tafa Stars?
JIBU: Siwezi kukasirika kwa sababu ya kuachwa Taifa Stars kwa sababu huo ni uamuzi wa kocha na lengo lake ni kuibua damu changa. Binafsi nampongeza kwa uamuzi wake huo kwa sababu ni mzuri na umelenga kujenga timu imara ya miaka ijayo.
SWALI: Wiki iliyopita Taifa Stars ilichapwa mabao 2-0 na Ivory Coast katika mechi yake ya kwanza ya michuano ya kuwania kufuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia za 2014. Umekipokeaje kipigo hicho?
JIBU: Ninachoweza kusema ni kwamba wachezaji wetu walijitahidi sana kucheza vizuri, lakini bahati haikuwa yetu. Lakini tukumbuke kwamba tulikuwa tukicheza na timu ngumu na inayoundwa na wachezaji wengi nyota duniani, hivyo kufungwa idadi hiyo ya mabao ugenini tulijitahidi sana.
Jambo la msingi ni kwa wachezaji wetu kujipanga upya kwa mechi zijazo ili tuweze kuibuka na ushindi na kufufua matumaini ya kusonga mbele. Uwezo tunao na nafasi ya kufanya hivyo ipo kwa sababu kocha wetu ni mzuri na malengo yake pia ni mazuri.
SWALI: Unadhani ni kipi kilichosababisha tufungwe na Ivory Coast katika mechi hiyo?
JIBU: Kama nilivyosema awali, tulifungwa kwa sababu wenzetu walitumia uzoefu wao katika mashindano ya kimataifa na walitumia vyema makosa yetu kupata mabao.
Inawezekana pia kuwa baadhi ya wachezaji wetu, hasa wale wapya kwenye kikosi cha Taifa Stars walicheza kwa hofu, japokuwa sio sana. Lakini hayo yote yameshapita, tugange yajayo.
Cha msingi ni kwa kocha kurekebisha dosari zilizojitokeza katika mechi hiyo na kujipanga vizuri kwa pambano letu lijalo dhidi ya Gambia, litakalochezwa wiki ijayo hapa nchini.
SWALI: Ulikuwemo kwenye kikosi cha Taifa Stars kilichocheza na Ivory Coast mwaka 2010 wakati ilipokuwa njiani kwenda Afrika Kusini kucheza fainali za Kombe la Dunia. Unadhani kiwango wanachocheza katika mechi za kirafiki za kimataifa ni sawa na kile wanachokionyesha katika klabu zao za Ulaya?
JIBU: Wanasoka wengi wa kiafrika wanaocheza Ulaya huwa ni waoga wa kuumia katika mechi za kirafiki na za michuano ya Afrika. Huwa wanacheza kwa uangalifu mkubwa na hawatumii nguvu nyingi kwa vile hawataki kuumia.
Nina hakika hata wachezaji wa Ivory Coast walicheza kwa staili hiyo katika mechi yao na Taifa Stars kama walivyofanya tulipocheza nao mwaka 2010 hapa nyumbani. Huwa wanatumia zaidi uzoefu na mbinu za kimataifa kushinda mechi zao.
Na hii ni kwa sababu, wanapoumia katika timu zao za taifa, hapatiwi huduma nzuri za matibabu kama inavyokuwa katika klabu zao za Ulaya. Wakati mwingine hata malipo wanayopewa huwa ni kidogo ndio sababu hawachezi kwa kujituma sana uwanjani.
Kingine ni kwamba, wachezaji wengi wanaocheza Ulaya huwa na jeuri ya aina fulani ndio sababu huwa wakikamiwa sana na wachezaji wa timu pinzani kwa lengo la kuwaonyesha kwamba hawana lolote la maana. Hali hiyo huwafanya wacheze kwa tahadhari kubwa.
Lakini ukweli ni kwamba Ivory Coast haina ngome imara na inaweza kupitika wakati wote wa mchezo. Nina hakika tutakapocheza nao katika mechi ya marudiano hapa nyumbani, tutaweza kuwaonyesha maajabu kwa vile wachezaji wetu watakuwa tayari wameshapata uzoefu mkubwa.
SWALI: Una maoni gani kuhusu soka ya Tanzania? Unadhani kipi kifanyike ili kuinua maisha ya wanasoka wa Tanzania?
JIBU: Ninaiomba serikali iangalie uwezekano wa kubadili mfumo wa uendeshaji soka nchini na kuanzisha soka ya kulipwa ili wachezaji wote waweze kunufaika na vipaji vyao.
Mfumo tunaotumia hivi sasa ni mbaya na umepitwa na wakati na hauwasaidii wachezaji kujenga maisha yao ya baadaye. Maisha ya wachezaji huwa mazuri pale wanapocheza soka, lakini wakishastaafu, wanakuwa na maisha mabaya sana.
Nadhani serikali inapaswa kusimamia na kuhakikisha kuwa, wachezaji wote wa Tanzania, hasa wanaocheza katika ligi kuu wanakatwa pesa zao na kupelekwa na mifumo ya kijamii kama vile NSSF ili fedha hizo zije kuwasaidia kwa maisha yao ya baadaye.
Nimejifunza mambo mengi sana tangu nilipoanza kucheza soka hadi leo hii na kubaini kwamba, mfumo tunaoendelea nao unatuumiza. Tunakuwa hatuna mawazo juu ya maisha yetu ya baadaye. Lazima tuanze sasa kuwaokoa wachezaji wetu kwa kuzilazimisha klabu kupeleka sehemu ya mishahara yao katika taasisi kama za NSSF.
SWALI: Ungependa kutoa ushauri gani kwa viongozi wa vyama na klabu za soka nchini?
JIBU: Nawaomba viongozi wa soka waongeze bidii katika kusaka maendeleo na kuibua vipaji vya vijana na ikiwezekana kuwawezesha kimaisha.
Umefika wakati kwa wachezaji na viongozi kila mmoja ufanya kazi yake kwa uhakika ili kuleta maendeleo ndani ya nchi kupitia soka. Pia tuwape nafasi wachezaji wetu ya kwenda kucheza soka ya kulipwa nje ya nchi.
Pia nawaomba viongozi wa serikali wawe wakali kwa watendaji, wanaouza sehemu za viwanja vya michezo kwa ajili ya kujenga nyumba za makazi na starehe. Tabia hii inachangia kudumaza maendeleo ya michezo kwa kuwafanya watoto wetu wakose nafasi za kuonyesha vipaji vyao.

No comments:

Post a Comment