KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, February 17, 2013

SIMBA YAWAPA MAJONZI MASHABIKI WAKE, YACHAPWA 1-0 NA WAANGOLA



SIMBA leo imeshindwa kuutumia vyema uwanja wake wa nyumbani baada ya kuchapwa bao 1-0 na Recreativo Libolo ya Angola katika mechi ya awali ya raundi ya kwanza ya michuano ya klabu bingwa Afrika iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam

Kipigo hicho kimeiweka Simba kwenye mazingira magumu ya kusonga mbele katika michuano hiyo kwa vile italazimika kushinda mechi ya marudiano kwa mabao 2-0. Mechi hiyo itachezwa wiki mbili zijazo nchini Angola.

Kimchezo, Simba haikuonekana kucheza kwa dhamira ya ushindi tangu mwanzo kutokana na wachezaji wake kutokuwa na kasi na kushindwa kucheza kwa malengo.

Bao pekee na la ushindi la Libolo lilifungwa na Joas Martis dakika ya 24 alipounganisha wavuni kwa kichwa krosi kutoka kwa Carlos Almeida.

Mshambuliaji Mrisho Ngasa ndiye pekee aliyeonekana kuisumbua ngome ya Libolo lakini alikosa ushirikiano kutoka kwa Amri Kiemba na Haruna Moshi Boban.

Mabadiliko yaliyofanywa na Kocha Patrick Liewig wa Simba katika kipindi cha pili yaliua kasi ya mchezo ya timu hiyo na kupokewa kwa hisia tofauti na mashabiki wa timu hiyo. Kocha huyo alimtoa Mussa Mudde, Haruna Chanongo na Haruna Moshi na kuwaingiza Amir Maftah, Ramadhani Singano na Salum Kinje.

Baadhi ya viongozi wa Simba waliokuwa wamekaa jukwaa la VIP walionekana wazi kupinga mabadiliko hayo, hasa wakati alipotolewa Boban.

Beki Juma Nyoso aliyekuwa amesimamishwa kwa makosa ya utovu wa nidhamu na Komabil Keita, ambaye alionekana kiwango chake kipo chini, walikuwa kizingiti kikubwa kwa washambuliaji wa Libolo kutokana na kucheza kwa uelewano mkubwa na kuosha mipira mingi ya hatari.

No comments:

Post a Comment