KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, February 25, 2013

SERIKALI YAITUNISHIA MISULI FIFA, TANZANIA HATARINI KUFUNGIWA



SERIKALI imeamuru mchakato wa uchaguzi mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) uanze upya kwa kufuata katiba ya 2006.

Uamuzi huo ulitangazwa jana na Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara alipozungumza na waandishi wa habari mjini Dar es Salaam.

Waziri Fenella alisema serikali imefikia uamuzi huo baada ya kubaini kuwa, katiba ya sasa ina mapungufu mengi na ilipitishwa bila kufuata katiba ya TFF.

Mbali na kutoa agizo hilo, Waziri Fenella alitangaza kumfuta kazi Msajili wa Vyama na Klabu za Michezo nchini, aliyepitisha katiba hiyo kwa madai kuwa alifanya hivyo kimakosa.

Uamuzi huo wa Waziri Fenella huenda ukasababisha Tanzania ifungiwe na Shirikisho la Soka la Dunia (FIFA) kwa vile katiba ya TFF inazuia serikali kuingilia kati masuala ya soka.

Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, hawajapata barua yenye agizo hilo kutoka kwa Waziri Fenella, lakini uamuzi huo unamaanisha kwamba, Tanzania ipo hatarini kufungiwa.

"FIFA imeshaelekeza wazi kwa wanachama wake kuwa, serikali haziruhisiwi kuingilia kati masuala ya soka kwa sababu vipo vyombo maalum vilivyopewa jukumu hilo kikatiba, sasa kama waziri ametoa agizo hilo, tusubiri tuone,"alisema.

Uchaguzi mkuu wa TFF ulisimamishwa baada ya kutokea mgogoro, kufuatia Kamati ya Rufani kumwengua Jamal Malinzi kugombea nafasi ya urais kwa madai kuwa hana uzoefu wa uongozi wa miaka mitano.

FIFA ilitangaza wiki iliyopita kuwa, itatuma wajumbe wake kuja nchini mwezi ujao kuchunguza mgogoro huo ikiwa ni pamoja na kuzihoji pande husika kabla ya kutoa uamuzi.

Hii ni mara ya pili kwa serikali kuingilia kati mgogoro ndani ya TFF, wakati huo kikijulikana Chama cha Soka nchini (FAT) na kusababisha Tanzania kabla ya serikali kusalimu amri.

No comments:

Post a Comment