KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Tuesday, July 17, 2012

Manji akutana na wachezaji wa Yanga leo

Mwenyekiti mpya wa Yanga, Yussuf Manji akisalimiana na mchezaji Athumani Iddi Chuji alipowatembelea na kukutana na wachezaji wa timu hiyo leo katika makao makuu ya klabu hiyo mitaa ya Twiga na Jangwani, Dar es Salaam.


Mwenyekiti wa Yanga, Yussuf Manji akizungumza na wachezaji wa timu hiyo alipokutana nao leo asubuhi makao makuu ya klabu hiyo mitaa ya Twiga na Jangwani, Dar es Salaam. (Picha zote na Emmanuel Ndege wa blogu ya liwazozito).


UONGOZI mpya wa klabu ya Yanga leo asubuhi ulitembelea makao makuu ya klabu hiyo mitaa ya Twiga na Jangwani, Dar es Salaam na kukutana na kuzungumza na wachezaji.
Viongozi hao wapya waliokuwepo kwenye msafara huo ni mwenyekiti, Yussuf Manji, makamu mwenyekiti, Clement Sanga na wajumbe wa kamati ya utendaji, Abdalla Bin Kleb, Mussa Katabalo na George Manyama.
Katika msafara huo, pia walikuwemo wajumbe wa kamati ya utendaji katika uongozi uliopita, Salum Rupia na Mohamed Bhinda.
Katika kikao chake hicho na wachezaji, Manji aliwataka wawe na imani kubwa kwa uongozi mpya kwa vile wamejipanga vyema kuhakikisha timu inapata huduma zote muhimu na kwa wakati na pia inapata ushindi katika kila mechi watakazocheza.
Manji aliwaeleza wachezaji hao kuwa, wanapaswa kucheza kwa ari na kujituma kwa vile matatizo yaliyojitokeza msimu uliopita hayatakuwa na nafasi katika uongozi wake.
Katika kikao hicho, wachezaji wa Yanga walionekana kuwa na furaha kubwa huku kila wakati wakipiga makofi ya kumshangilia mfadhili huyo wa zamani wa klabu hiyo.
Mbali na Manji, viongozi wengine waliopata nafasi ya kuzungumza na wachezaji ni Sanga na Katabalo, ambao waliwaelezea mikakati mbalimbali ya uongozi wao.
Manji alichaguliwa kuwa mwenyekiti mpya wa Yanga mwishoni mwa wiki iliyopita baada ya kuwabwaga Edgar Chibula na John Jambele. Uchaguzi huo ulifanyika kwenye ukumbi wa Diamond, Jubilee, Dar es Salaam.
Uchaguzi huo mdogo uliitishwa baada ya kujiuzulu kwa mwenyekiti wa zamani wa klabu hiyo, Lloyd Nchunga, makamu wake, Davis Mosha na wajumbe wanne wa kamati ya utendaji huku mmoja akifariki dunia.



No comments:

Post a Comment