KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Tuesday, July 10, 2012

EL SALAM WAU, ATLETICO ZAWASILI DAR KWA KAGAME

El Salam Wau ya Sudan Kusini na Atletico ya Burundi zinatarajiwa kuwa timu za kwanza kuwasili nchini kushiriki michuano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati (Kombe la Kagame).
Michuano hiyo inaanza kutimua vumbi Jumamosi (Julai 14 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam ikishirikisha timu kumi na moja akiwemo bingwa mtetezi Yanga na makamu bingwa Simba.
Kikosi cha El Salam Wau ambacho kitawasili kesho alfajiri (Julai 11 mwaka huu) kwa ndege ya Ethiopia Airlines kikitokea Juba kupitia Addis Ababa, Ethiopia kikiwa na wachezaji 18 na viongozi saba.
Wachezaji wanaounda kikosi hicho ni Khamis Leone Uso Wani (nahodha), Adheil Bugwic Jongkor Bugwic, Edward Joram Simon Julio, Fidel Andrea Fides Fas, Ismael Musa Juma Ismael, James Anei Matheli Anei, Jervas Ayo Abdalla Ayak, Khamis Doshama Ulama Andel na Meki Sultan Berema Kuku.
Wengine ni Moga Emmanuel Androga, Mubarak Mohammed Saleh Omer, Ndili Rabeh Nasir Hozi, Nizir Rihan Taban Talib, Oliver Paul Kangi Akok, Rabie Mohammed Abubakar Hassan, Rufino Joseph Uras Ambros, Santino Makuei Uyu Upio, Thomas Rufino Thomas Diakon.
Nayo Atletico inatarajiwa kuwasili kesho (Julai 11 mwaka huu) kwa usafiri wa barabara. Timu hiyo inakuja kwa usafiri wa basi lake ambalo pia italitumia kwa muda wote itakapokuwa kwenye mashindano.
Wakati El Salam Wau itafikia kwenye hoteli ya Rungwe iliyoko maeneo ya Kariakoo, Atletico itakuwa Lunch Time Hotel iliyoko Mabibo.
Timu zinazotarajiwa kuwasili keshokutwa (Julai 12 mwaka huu) ni Mafunzo ya Zanzibar kwa boti saa 9 alasiri, Vita Club ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (RDC) itatua saa 1.20 usiku kwa Kenya Airways. Timu nyingine itakayowasili siku hiyo jioni ni URA ya Uganda.
WATANGAZAJI KWA ‘SCREEN’ KUBWA KOMBE LA KAGAME
Wakati wa michuano ya Kombe la Kagame itakayofanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia Julai 14-28 mwaka huu, screen kubwa iliyoko uwanjani itatumika kwa matangazo ya biashara na ujumbe mbalimbali kwa washabiki watakaoshuhudia mechi hizo.
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linakaribisha kampuni na wadau mbalimbali wanaotaka kuweka matangazo yao wakati wa michuano hiyo itakayoshirikisha klabu kumi na moja kutoka ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kati.
Muda wa kurushwa matangazo hayo yanayotakiwa kuwa kwenye mfumo wa DVD ni kabla ya mechi kuanza, wakati wa mapumziko na baada ya mechi. Matangazo hayo yanatakiwa kuwa ya sekunde 60 (dakika moja) au sekunde 30 (nusu dakika).

No comments:

Post a Comment