KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Friday, November 30, 2012

UGANDA YAUA



UGANDA imefuzu kwa asilimia 100 hatua ya Robo Fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Tusker Challenge baada ya kushinda mechi zake zote za Kundi A, ikiwemo ya leo waliyoshinda 4-0 dhidi ya Sudan Kusini.

Hakuna mjadala, Sudan Kusini inaondoka katika mashindano haya, bila kuingiza hata pointi moja, wakifungwa mechi zote tatu.Uganda na Kenya wamefuzu moja kwa moja, wakati Ethiopia walioshika nafasi ya tatu watasubiri hatima yao kufuzu kama mmoja wa washindi wa watatu bora kutoka makundi yote, A, B na C.

Katika mchezo wa leo, mabao ya Uganda ambao pia ni mabingwa watetezi yalifungwa na Brian Umony mawili katika dakika za 23 na 39, Robert Ssentongo dakika ya 47 na Hamisi Kiiza ‘Diego’ dakika ya 79.

Katika mechi ya kwanza, Kenya ilishinda 3-1 dhidi ya Ethiopia, mabao ya Ramadhan Mohamed Salim, Clifton Miheso na David Ochieng, wakati la Ethiopia lilifungwa na Gatech Panom Yietch.

Michuano hiyo, itaendelea kesho kwa mechi za Kundi B na C, saa 8:00 mchana, Tanzania Bara watamenyana na Somalia Uwanja wa Lugogo na baadaye saa 10:00, Rwanda itacheza na Eritrea wakati Sudan itaanza na Burundi saa 8:00 mchana Uwanja wa Wankulunkulu na baadaye saa 10:00 jioni Malawi watamenyana na Zanzibar Wankulunkulu.

Kikosi cha Uganda kilikuwa; Ali Kimera, Robert Ssentongo, Joseph Ochaya, Kweyune Said, Henry Kalungi, Isaac isinde, Manco Kaweesa/Joseph Mpande, Geoffrey Kizito, Nico Wakiro Wadada, Brian Umony/Brian Majwega na Hamisi Kiiza.

No comments:

Post a Comment