KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, November 22, 2012

RAGE: HATUNA MATATIZO NA FRIENDS OF SIMBA, HANSPOPE ATAKA MKUTANO WA DHARULA





Mwenyekiti wa klabu ya Simba, Ismail Aden Rage amesema uongozi wake hauna ugomvi wala matatizo na kundi la wanachama, maarufu kwa jina la Friends of Simba.
Rage amesema wanawaheshimu baadhi ya wanachama wa kundi hilo kwa sababu wamekuwa wakitoa mchango mkubwa kwa maendeleo ya klabu.
Hata hivyo, Rage amesema wapo baadhi ya wanachama wa kundi hilo, ambao hawautakii mema uongozi wake kwa vile wamekuwa wakishirikiana na makundi ya wanachama kuchochea vurugu.
Alisema kinachosikitisha ni kwamba, wanachama wa kundi hilo wanawafahamu vyema wenzao wachache wenye lengo la kuchochea vurugu, lakini hakuna hatua zozote walizowachukulia.
Rage amesema iwapo hali itaendelea kuwa hivyo, uongozi wake utalazimika kuwataja wanachama hao ili wafahamike na wahukumiwe kutokana na matendo yao.
"Si kweli kabisa kwamba uongozi wa Simba hauelewani na wanachama wa Friends of Simba. Tunawaheshimu sana kwa sababu baadhi yao wamekuwa wakitumia fedha zao nyingi kwa manufaa ya Simba,"alisema Rage.
"Lakini wapo baadhi ya wanachama wa kundi hilo miongoni mwao, ambao wamekuwa mstari wa mbele kuchochea vurugu kupitia katika baadhi ya matawi, lengo lao kubwa likiwa ni kuuondoa uongozi uliopo madarakani ili wakae wao,"aliongeza.
Akizungumzuia ombi la kuitishwa kwa mkutano wa dharula, Rage alisema uongozi wake hauna kinyongo na ombi hilo la wanachama, isipokuwa wanapaswa kufuata taratibu na katiba ya klabu hiyo.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa kamati ya usajili ya Simba, Zacharia Hanspope amesema suluhusho pekee la mgogoro uliojitokeza sasa Simba ni kuitishwa kwa mkutano wa dharula wa wanachama ili waweze kujadili matatizo yaliyojitokeza na kuchukua hatua.
Alisema baadhi ya wanachama wa friends of Simba, akiwemo yeye wamekuwa wakiisaidia klabu hiyo kwa mapenzi yao wenyewe na katu hawana malengo ya kutaka uongozi.
Hata hivyo, alisema anashangaa kuona kuwa, wanachama hao hawakusema lolote katika mkutano ulioitishwa na uongozi hivi karibuni, badala yake wanazusha hoja ya kutaka uitishwe mkutano wa dharula hivi sasa.

No comments:

Post a Comment