KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, March 7, 2013

KUMEKUCHA KOMBE LA NSSF



MABINGWA watetezi wa michuano ya soka ya Kombe la NSSF, Habari Zanzibar wamepangwa kufungua dimba la michuano hiyo mwaka huu kwa kumenyana na Changamoto.

Mratibu wa michuano hiyo, Juma Kintu alisema jana kuwa, mechi hiyo ya ufunguzi imepangwa kuchezwa keshokutwa kuanzia saa mbili asubuhi kwenye uwanja wa klabu ya Sigara, Chang'ombe, Dar es Salaam.

Kintu alisema katika michuano ya netiboli, wenyeji NSSF watafungua dimba kwa kumenyana na Mlimani. Mechi hiyo pia imepangwa kuchezwa keshokutwa kuanzia saa 1.30 asubuhi.

Kwa mujibu wa Kintu, mgeni rasmi katika sherehe za ufunguzi wa michuano hiyo anatarajiwa kuwa Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudencia Kabaka.

Kintu alisema michuano hiyo inatarajiwa kuendelea Jumapili kwa mechi moja ya soka kati ya TSN na Free Media, itakayochezwa kuanzia saa mbili asubuhi.

Alisema michuano hiyo itaendelea Machi 11 mwaka huu kwa mechi mbili. Katika mechi ya kwanza itakayochezwa uwanja wa Sigara, NSSF itamenyana na Redio Heri na katika mechi ya pili itakayochezwa uwanja wa DUCE, BTL itacheza na IPP.

Machi 12, Uhuru Media itavaana na Mlimani kwenye uwanja wa Sigara wakati Free Media itamenyana na Tumaini kwenye uwanja wa Duce.

Machi 13, Jambo Leo itamenyana na Global kwenye uwanja wa Sigara wakati TBC itamenyana na New Habari kwenye uwanja wa Duce.

Machi 14, Mwananchi itamenyana na Sahara Media kwenye uwanja wa Sigara wakati TSN itamenyana na Tumaini kwenye uwanja wa Duce.

Kwa upande wa netiboli, michuano hiyo itaendelea Machi 11 wakati TBC watakapomenyana na Sahara kuanzia saa 10 jioni kabla ya Uhuru kuvaana na Free Media kuanzia saa 11 jioni.

Machi 12, IPP itamenyana na Jambo Leo kabla ya BTL kuonyeshana kazi na Changamoto. Machi 13, Mwananchi itacheza na New Habari kabla ya Global kumenyana na Tumaini.

Mratibu huyo alisema michuano ya mwaka huu itachezwa kwa mtindo wa mtoano kutokana na muda wa kufanyika kwake kuwa mfupi.

Alisema mechi za fainali za michuano hiyo zimepangwa kuchezwa Machi 23 mwaka huu kwenye uwanja wa Sigara.

No comments:

Post a Comment