KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Saturday, March 9, 2013

HABARI ZANZIBAR YAVULIWA UBINGWA KOMBE LA NSSF



Meneja Kiongozi wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF),  Eunice Chiume (kushoto) akikabidhi jezi kwa kiongozi wa klabu ya michezo ya Uhuru Media, Rashid Zahor wakati wa hafla ya makabidhiano ya vifaa vya michezo kwa timu zitakazoshiriki michuano ya Kombe la NSSF iliyofanyika jana makao makuu ya shirika hilo mjini Dar es Salaam. Wengine pichani ni katibu wa kamati ya mashindano hayo, Modest Msangi na mratibu, Juma Kintu. (Picha na Emmanuel Ndege).

MABINGWA watetezi wa michuano ya soka ya Kombe la NSSF, Habari Zanzibar jana walivuliwa ubingwa baada ya kupigwa mweleka wa mabao 3-0 na Changamoto.

Katika mechi hiyo ya ufunguzi iliyochezwa kwenye uwanja wa klabu ya Sigara, Chang'ombe, Dar es Salaam, Changamoto ilikwenda mapumziko ikiwa mbele kwa bao 1-0.

Bao la kwanza la Changamoto lilipachikwa wavuni na Ahmed Ganichaga dakika ya 20 kabla ya Hashim Kimbaga na Lutende Mwakalule kuongeza mengine mawili dakika ya 78 na 84.

Kutokana na kipigo hicho, Habari Zanzibar imetolewa katika michuano hiyo inayochezwa kwa mtindo wa mtoano wakati Changamoto imefuzu kucheza robo fainali.

Katika michuano ya netiboli, wenyeji NSSF walianza kwa kishindo na kutoa onyo kwa timu zingine baada ya kuicharaza Mlimani TV mabao 46-1.

Wafungaji wa mabao ya NSSF walikuwa Pili Singano, aliyefunga 22 na Sifa Katila aliyefunga mabao 24.

Akifungua michuano hiyo, Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudencia Kabaka aliipongeza NSSF kwa kuwakutanisha wafanyakazi wa vyombo vya habari kupitia mashindano hayo.

Alisema mashindano hayo ni muhimu kwa vile yanajenga uhusiano mzuri kati ya vyombo vya habari na pia yanawaweka wafanyakazi wa vyombo hivyo katika afya nzuri.

Viongozi wengine waliohudhuria hafla ya ufunguzi wa michuano hiyo ni Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Dk. Ramadhani Dau na Meneja Kiongozi, Uhusiano wa shirika hilo, Eunice Chiume.

Michuano hiyo inaendelea tena leo wakati Free Media itakapomenyana na TSN kwenye uwanja wa Sigara kuanzia saa mbili asubuhi.

Kesho, IPP itashuka dimbani kumenyana na TBL kwenye uwanja wa Sigara wakati NSSF itamenyana na Redio Kheri kwenye uwanja wa DUCE.

Katika netiboli, TBC itamenyana na Sahara kuanzia saa 10 jioni kabla ya Uhuru Media kumenyana na Free Media kuanzia saa 11 jioni.

No comments:

Post a Comment