KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Sunday, March 31, 2013

NANCY SUMARI: KUJIAMINI KUMENIFIKISHA NILIPO



MREMBO wa Tanzania wa 2005, Nancy Sumari amesema kufanya kitu bila kuogopa kushindwa ndio siri ya kufanikiwa kwake katika mambo mbalimbali.

Akihojiwa katika kipindi cha Makutano kilichorushwa hewani wiki iliyopita kupitia kituo cha televisheni cha DTV, Nancy alisema katika maisha yake, haogopi kufanya kitu chochote hata kama hana uzoefu nacho.

Nancy alisema utamaduni wake huo wa kujiamini ndio uliomwezesha kushinda mataji ya Miss Dar Indian Ocean, Miss Kinondoni na hatimaye Miss Tanzania.

Mbali na kutwaa mataji hayo, Nancy pia alikuwa Mtanzania wa kwanza kuweka rekodi ya kushinda taji la Miss World Africa 2005 baada ya kufuzu kuingia hatua ya fainali.

Mama huyo wa mtoto mmoja alisema, kabla ya kujitosa katika mashindano ya urembo, aliwahi kufanyakazi kama muuzaji katika duka la fenicha na kulipwa mshahara wa sh. 120,000 kwa mwezi.

Alisema aliamua kufanyakazi hiyo baada ya kukwama kupata nafasi ya kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kitivo cha sheria, kutokana na chuo hicho kutoruhusu mwanafunzi aliyemaliza kidato cha nne kwa elimu ya Kenya, kujiunga moja kwa moja kwa masomo ya shahada.

"Nilifanyakazi hiyo kwa moyo wote hadi nilipopata nafasi ya kushiriki mashindano ya urembo baada ya waandaaji kuniona na kuvutiwa na mimi,"alisema.

Akizungumzia uamuzi wake wa kuchapisha kitabu cha Nyota Yako, Nancy alisema umetokana na kutokuta vitabu vya watoto madukani vilivyoandikwa na waandishi wa Tanzania.

"Mbali ya kuwa mimi ni mama kwa wakati huu, kila nilipokwenda kwenye maduka ya vitabu, nilikosa vitabu vya watoto vilivyoandikwa na waandishi wa Tanzania. Vingi vimeandikwa na waandishi wa nje,"alisema.

"Hivyo niliamua kuandika kitabu, ambacho watoto wa kike wa Tanzania wataweza kukisoma na kuvutiwa kufanya kile, ambacho nimekiandika kwenye kitabu hicho,"aliongeza.

Kwa mujibu wa Nancy, kitabu hicho kinapatikana katika maduka ya Scholastica lililopo Mlimani City na Novel Idea lililopo Masaki, Dar es Salaam kwa bei ya sh. 5,000.

Nancy amewataka vijana wanaochipukia kujaribu kuwa wazuri kwa sababu kila mmoja anafanya makosa, hakuna aliye sahihi kwa asilimia 100.

"Lakini ni muhimu kama binadamu, tujitahidi kufanya vitu sahihi, sawa na unapoona ua linafifia, limwagilizie maji likue na unapomwona mwenzako anahitaji msaada na unayo nafasi, usisite kumsaidia,"alisema.

Nancy kwa sasa ni Mkurugenzi wa Matukio wa Kampuni ya Frontline Management, ambayo amekuwa akiiongoza kwa kushirikiana na mrembo mwenzake, Irene Kiwia na anatarajia kumaliza masomo ya Chuo Kikuu Julai mwaka huu.

No comments:

Post a Comment