KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Monday, March 25, 2013

STARS, MOROCCO ZAINGIZA MILIONI 226

MECHI ya mchujo ya Kombe la Dunia kati ya Tanzania, Taifa Stars na Morocco, Simba wa Atlas iliyochezwa jana na wenyeji kuibuka na ushindi wa mabao 3-1 imeingiza Sh. 226,546,000.

Fedha hizo zimepatikana kutokana na watazamaji 32,614 waliokata tiketi
kushuhudia mechi hiyo kwa kiingilio cha sh. 5,000, sh. 7,000, sh. 10,000, sh. 15,000, sh. 20,000 na sh. 30,000.

Mgawanyo wa mapato hayo ulikuwa kama ifuatavyo; asilimia 18 ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ni sh. 34,557,864.41, maandalizi ya mchezo Sh. 28,450,000 wakati wa gharama za uchapaji tiketi ni sh. 8,625,641.88.

Nyingine ni bonasi kwa timu ya Taifa Stars sh. 28,798,220.34, asilimia 15 ya uwanja sh. 18,917,141.01, asilimia 20 ya gharama za mechi sh. 25,222,854.67 na asilimia 5 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) sh. 6,305,713.67.

Asilimia 60 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) sh. 71,885,135.82 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 3,783,428.20 ambayo ni asilimia 5 kutoka kwenye mgawo wa TFF.

Katika hatua nyingine, Rais wa TFF, Leodegar Tenga amewapongeza wachezaji wa Taifa Stars na benchi lao la ufundi,washabiki, mdhamini na Serikali kwa kufanikisha ushindi wa jana.

Tenga amesema ushindi huo umetokana na ushirikiano kutoka kwa wadau wote, na hasa wachezaji walioonesha kiwango kikubwa kulinganisha na mechi zilizopita ikiwemo kiwango cha kujituma uwanjani.

Amesema Serikali ni mdau mkubwa wa mpira wa miguu katika miundombinu, usalama na idara zake mbalimbali ikiwemo Uhamiaji ambayo imefanikisha kwa kiasi kikubwa kuwepo kwa mechi hiyo.

No comments:

Post a Comment