KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, October 24, 2012

BOBAN, NYOSO WASIMAMISHWA SIMBA



SIMBA SPORTS CLUB
P.O.BOX 15318
TEL+255 222183330
FAX +255 222183330
MSIMBAZI/MCHIKICHI STREET
DAR ES SALAAM
TANZANIA
EMAIL simbasportsclub@yahoo.com
WEBSITE www.simba.co.tz
AFFILIATED TO TFF, DRFA and IDFA
24/10/2012
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
KLABU ya soka ya Simba inapenda kutoa taarifa zifuatazo kwenu siku ya leo.
1. Kuhusu Boban na Nyoso
Wachezaji wawili wa Simba, Haruna Moshi Shaaban (Boban) na Juma Said Halfan (Nyoso), wamesimamishwa kuitumikia timu ya wakubwa (senior) kwa sababu na nyakati tofauti.
Moshi amesimamishwa kuichezea timu ya wakubwa kutokana na vitendo vya utovu wa nidhamu na kutokuwa na heshima kwa mwajiri (timu). Klabu imempa Haruna muda wa siku 21 kutoa maelezo kuhusu makosa yake na iwapo atashindwa kutoa maelezo ya kuridhisha, klabu inaweza kumchukulia hatua zaidi.
Katika kipindi hicho (siku 21 kuanzia jana), Boban atapokea nusu ya mshahara wake wa kila mwezi na hatapata marupurupu yoyote yanayohusiana na timu ya wakubwa.
Kwa upande wa Nyoso, uongozi umemwagiza afanye mazoezi na kikosi cha timu ya pili (Simba B) hadi hapo atakapoimarisha kiwango chake cha uchezaji.
Hatua hii imetokana na ripoti ya benchi la ufundi iliyoonyesha kwamba mchezaji huyo amekuwa akifanya makosa mengi ya kiuchezaji yanayoigharimu na ingawa amekuwa akipewa maelekezo na walimu, bado amekuwa akirudia makosa yaleyale.
Kutokana na hilo, Nyoso atafanya mazoezi na wachezaji wa kikosi cha pili hadi walimu watakaporidhika kwamba amejirekebisha na yuko tayari kutumikia kikosi cha wakubwa.
Katika muda wake wote huo akifanya mazoezi na timu B, Nyoso atakuwa akipata mshahara wake wa kila mwezi kama kawaida na pia atapata marupurupu wanayopata wachezaji wa Simba B.

Emmanuel Okwi
Klabu ya Simba inaeleza kusikitishwa kwake na taarifa za vyombo vya habari vyenye lengo la kuuza magazeti pasipo kujali athari za habari zenyewe.
Kwa mfano, habari ya kwenye gazeti la CHAMPIONI la leo ina kichwa cha habari KATIBU MKUU AMFUKUZA OKWI SIMBA. Hata hivyo, kilichoandikwa ndani ya habari yenyewe kinamnukuu aliyewahi kuwa Katibu Mkuu kwenye miaka ya nyuma.
Gazeti hilo linafahamu kabisa kwamba Simba ina Katibu Mkuu mmoja tu kwa sasa na anaitwa Evodius Mtawala. Simba haijawahi kuwa na makatibu wakuu wawili kwa wakati mmoja.
CHAMPIONI linafahamu ukweli huu lakini kwa sababu inazozijua lenyewe, imeamua kuandika habari hiyo na kuweka kichwa cha habari cha namna hiyo pasipo kujali athari zake kwa wanachama wa Simba, Katibu Mkuu aliyepo madarakani kwa sasa na weledi wa fani ya uandishi wa habari
Kilichoandikwa kwenye habari hiyo ya CHAMPIONI ni maoni binafsi ya mwanachama wa Simba na kwa mujibu wa Katiba ya Tanzania, kila mtu ana uhuru wa kutoa maoni yake kuhusiana na jambo lolote ali mradi halivunji sheria za nchi.
Simba SC inarudia wito wake wa kuvitaka vyombo kubaki kwenye misingi ya kitaaluma na kuacha kuandika habari zilizotiwa chumvi na kuleta mitafuruku isiyo na sababu yoyote.

Kikosi
Simba inaendelea vizuri na mazoezi visiwani Zanzibar kujiandaa na mechi dhidi ya Azam itakayopigwa katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam Jumamosi hii.
Hata hivyo, mchezaji Salim Kinje ameruhusiwa kuondoka kambini Zanzibar leo kutokana na kupata msiba wa baba yake mkubwa uliotokea Dar jana.
Uongozi, kwa namna ya kipekee kabisa, unatoa salamu za pole kwa familia ya Kinje kutokana na msiba huu.

Boniface Wambura
Kwa niaba yangu binafsi na klabu ya Simba, napenda kumpongeza Ofisa Habari wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Boniface Wambura, kwa kuteuliwa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) kuwa miongoni mwa wasimamizi wa shirikisho hilo katika michuano ya Wanawake itakayofanyika nchini Guinea ya Ikweta (Equatorial Guinea).
Wambura ndiye Mtanzania pekee aliyeteuliwa na CAF kutumika kwenye michuano hiyo na jambo hilo ni la faraja kwa tasnia ya habari nchini ambako Wambura ametokea.
Imetolewa na
Ezekiel Kamwaga
Ofisa Habari
Simba SC







No comments:

Post a Comment