KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, March 29, 2012

Wacheza shoo watakaocheza nusu uchi kukiona cha moto

BARAZA la Sanaa la Taifa (BASATA) limesema bado linakerwa na tabia ya uvunjifu wa maadili katika sanaa za maonyesho, hasa unenguaji na kutaka hali hiyo ifike mwisho.
Katibu Mtendaji wa BASATA, Ghonche Materego alisema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita mjini Dar es Salaam na kuongeza kuwa, ni lazima kuwe na mabadiliko dhidi ya uvunjifu wa maadili kwenye sekta ya sanaa, vinginevyo hatua zitaanza kuchukuliwa.
“Haya si mambo yanayofurahisha, ni lazima jamii ionyeshe ushirikiano kwa kupambana na udhalilishaji wa aina hii. Kuna mambo yasiyopaswa kufanyika hadharani na yanabaki kuwa ya ndani tu kwenye klabu za usiku na Casino, si vinginevyo” alisistiza Materego.
Aliongeza kuwa, si jambo la busara hata kidogo kwa maonyesho hayo ya sehemu maalum za ndani kuanza kufanywa hadharani kwani ni kinyume cha sheria na taratibu za nchi na ni udhalilishaji wa sekta ya sanaa hivyo aliwataka wasanii kujipanga ili kupambana na tatizo hilo.
“Mabadiliko lazima yafanywe. Vyama, mashirikisho na mitandao ya wasanii vianze mara moja kuangalia maadili kwenye maeneo yao. Hatua madhubuti zichukuliwe dhidi ya watakaoendelea kuvunja maadili kwenye sanaa” alisisitiza Materego.
Awali, Mwenyekiti wa Chama cha Muziki wa Dansi Tanzania (CHAMUDATA), Juma Ubao alisema kinachofanyika sasa kwenye unenguaji si muziki wa dansi bali ni aina fulani ya matukio ambayo ni maalum kwa ajili ya klabu za usiku.
“Unenguaji wa uchi usihusishwe hata kidodo na muziki wa dansi. Haya yanayofanyika sasa ni kuuchafua muziki huu. Ni lazima tuelewe haya si ya kuyavumilia kwenye muziki wetu” alisisitiza Ubao.
Alisema katika miaka ya nyuma, wanenguaji walikuwa wakivaa mavazi ya heshima na kufanya maonesho yaliyowavutia mashabiki wa rika zote, lakini kwa sasa hali ni tofauti kutokana na kuwepo kwa vikundi vinavyovaa uchi na kuanza kunengua hadharani.
Kwa upande wake, mtendaji kutoka asasi ya Binti Leo, inayojishughulisha na sanaa za majukwani, Betty Kazimbaya alisema, kinachofanyika sasa ni kudhalilisha sanaa na ukiukwaji wa maadili kupitia wasanii wanaolipwa pesa kiduchu hivyo kutaka hatua kali zichukuliwe.
“Kazi kubwa ya wasanii wa aina hii ni kusitiri mwili, inakuaje kuwe na vikundi havitumii mavazi haya kwa kazi hiyo?" Alihoji Kazimbaya

No comments:

Post a Comment