KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, March 22, 2012

SINTA: Tujitambue, kujiamini na kujithamini


MSANII machachari wa filamu za kibongo, Christina Manongi ‘Sinta’ amewataka wasanii wa kike nchini kujitambua na kujithamini badala ya kuwa waoga wa kuonyesha vipaji vyao.
Sinta amesema iwapo msanii wa kike atashindwa kujitambua mapema, ni rahisi kwake kutumiwa kimapenzi na wanaume hata kama anacho kipaji cha fani anayoshiriki.
Msanii huyo, ambaye alikuwa kimya kwa muda mrefu, alisema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita alipokuwa akihojiwa katika kipindi cha blogu yetu kilichorushwa hewani na kituo cha televisheni cha DTV.
“Msanii wa kike anapaswa kutambua kuwa, yeye ndiye baba na mama, akitaka kuwa kama Sinta, akiwa na moyo huo, atafanikiwa, vinginevyo utatongozwa na kutembea hovyo na wanaume,”alisema.
Sinta alisema binafsi alifanikiwa kujitosa kwenye fani ya filamu kutokana na uwezo na nguvu zake na kuongeza kuwa, kamwe hakuwahi kutumiwa na wanaume kwa jambo lolote.
Msanii huyo wa zamani wa kundi la sanaa la Kaole, alianza kujitosa kwenye fani ya filamu mwaka 2002, ambapo alishiriki kucheza filamu mbalimbali za kundi hilo.
Mbali na filamu, Sinta alishiriki kucheza tatmthilia kadhaa za kundi hilo zilizokuwa zikionyeshwa kupitia kituo cha televisheni cha ITV.
Sinta amekiri kuwa, japokuwa yamekuwepo mabadiliko makubwa katika fani hiyo hivi sasa, lakini zipo dosari nyingi, zikiwemo za baadhi ya wasanii kutokuwa na vipaji na uelewa wa fani hiyo.
Alisema baadhi ya wasanii wamejitosa kwenye fani ya filamu kutokana na kukosa la kufanya na wengine wanaiona fani hiyo kuwa ni nyepesi kuliko zingine.
“Hivi sasa kila mtu anataka kuwa mwigizaji. Ameshindwa kule, anataka uigizaji. Fani hii inataka kipaji zaidi, vingine vinafuata baadaye,”alisema.
Mwanadada huyo alisema anavutiwa zaidi na filamu za kiafrika, hasa za Kinigeria kwa sababu zinaelezea mazingira na hali halisi ya maisha ya kiafrika kuliko filamu za Hollywood.
Sinta alisema anamshukuru Mungu kwamba mpenzi wake wa sasa anamuelewa na kumwamini kwa kila kitu ndio sababu anaweza kufanya mambo yake bila kukumbana na vikwazo vyovyote.
“Nimekuwa nikipata mialiko mingi na wakati mwingine napata kazi za usiku, lakini kwa vile mpenzi wangu ni mwelewa, sipati matatizo,”alisema.
Alizitaja changamoto pekee, ambazo amekuwa akizipata katika maisha yake ya usanii kuwa ni kudharauliwa na baadhi ya watu bila ya kuwa na sababu za msingi.
Hata hivyo, alisema hakatishwi tamaa kutokana na dharau hizo kwa sababu anajiamini na siku zote humweka mbele Mungu na kusali kabla ya kufanya kitu chochote.
Kwa sasa, Sinta anajiandaa kuziingiza sokoni filamu zake mbili mpya. Alizitaja filamu hizo kuwa ni The return of J-LO na Sitaki demu.
Alisema filamu ya The return of J-LO inahusu mchezo wa soka na amewashirikisha wacheza soka kadhaa kama vile Emmanuel Okwi, Jerry Tegete na Amir Maftah.
Katika filamu ya Sitaki demu, amemshirikisha mpenzi wake wa zamani, msanii Juma Nature pamoja na wanasiasa Ridhiwani Kikwete na Zitto Kabwe.
Alisema filamu hizo ni tofauti na zile zilizozoeleka kwa sababu ameamua kutoka upya akiwa na vitu vipya. Alisema kama ni hadithi, nyingi zimeshatengenezewa filamu hivyo ni bora kutoka na mwonekano mpya.

No comments:

Post a Comment