KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Wednesday, March 14, 2012

Simba yaipigia hesabu ES Setif

UONGOZI wa klabu ya Simba umesema umeanza kuchukua tahadhari kubwa kabla ya kupambana na ES Setif ya Algeria katika mechi ya raundi ya pili ya michuano ya Kombe la Shirikisho.
Makamu Mwenyekiti wa Simba, Geofrey Nyange ‘Kaburu’ alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, miongoni mwa tahadhari hizo ni pamoja na kuhakikisha kuwa, wachezaji wao nyota hawaumii kabla ya mechi hiyo.
Simba na ES Setif zinatarajiwa kumenyana Machi 25 mwaka huu katika mechi itakayopigwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kurudiana wiki mbili baadaye mjini Algiers.
Kaburu alisema wamemwelekeza Kocha Mkuu wa timu hiyo, Milovan Cirkovic kupanga wachezaji kwa uangalifu ikiwa ni pamoja na kuwapumzisha baadhi ya nyota wao katika mechi za ligi kuu.
Alizitaja tahadhari nyingine walizochokua kuwa ni kuwaasa wachezaji wao kuepuka kucheza rafu za kizembe ili wasionyeshwe kadi nyekundu ama kufungiwa kucheza ligi.
Alisema wamepata funzo kubwa kutokana na vurugu zilizotokea wakati wa mechi ya ligi kuu kati ya Yanga na Azam, ambazo zilisababisha wachezaji watano wa timu hiyo ya Jangwani kufungiwa kucheza soka kwa nyakati tofauti.
Kaburu alikiri kuwa, mechi kati yao na ES Setif itakuwa ngumu kwa vile wapinzani wao ni wazoefu wa mashindano ya kimataifa na kikosi chao kinaundwa na wachezaji wengi nyota.
Alisema tayari wameshapata taarifa za kutosha kuhusu timu hiyo ya Algeria na wameshaanza kuzifanyiakazi kwa lengo la kuhakikisha wanaibuka na ushindi katika mechi hiyo.
Simba imepanga kucheza na ES Setif kuanzia saa tisa alasiri ili kuwachosha wapinzani wao, ambao hali ya hewa kwao ni baridi kali.
Tegemeo kubwa la Waalgeria ni nyota wake, Sofiene Zaaboub, ambaye ni raia wa Ufaransa, Kouamé Valentin kutoka Burkina Fasso, Youssef Sofiane na Akram Djahnit, ambao ni raia wa Algeria.

No comments:

Post a Comment