KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, March 29, 2012

JULIO: Tutaizika Yanga Mkwakwani




WAKATI homa ya pambano la ligi kuu ya soka kati ya Yanga na Coastal Union ikiwa imeshaanza kupanda, Kocha Mkuu wa Wagosi wa Kaya, Jamhuri Kihwelu ‘Julio’ ametamba kuwa watawasambaratisha wapinzani wao katika mechi hiyo. Katika makala hii iliyoandikwa na Mwandishi Wetu ATHANAS KAZIGE, kocha huyo anaelezea mikakati yao katika mechi hiyo na mambo mengine kadhaa.

SWALI: Kikosi chako kinatarajiwa kushuka dimbani Jumamosi ijayo kucheza na Yanga katika mechi ya ligi kuu ya Tanzania Bara, itakayochezwa kwenye Uwanja wa Mkwakwani mjini Tanga. Hebu tueleze mmejiandaaje kwa ajili ya mechi hiyo.
JIBU: Kikosi changu kipo fiti na hakuna mchezaji yeyote, ambaye ni majeruhi. Tuna uhakika mkubwa wa kuchukua pointi zote tatu kutoka kwa Yanga kwa sababu nimerudi na mbinu mpya za soka kutoka Arabuni, ambako nilikwenda miezi michache iliyopita.
SWALI: Kwa nini unajiamini sana kwamba mtaishinda Yanga?
JIBU: Nasema hivyo kwa sababu kikosi changu kipo imara na ninataka Yanga waingie uwanjani na kikosi chao chote pamoja na viongozi wao wote, lakini lazima tutawafunga.
Vilevile nimeshazisoma mbinu zao zote, hivyo suala la kuifunga Yanga halina mjadala, uhakika wa kuifunga ni mkubwa sana, hata kama mwamuzi atakuwa mwenyekiti wao, Lloyd Nchunga.
Kwangu mimi ninachoweza kusema ni kwamba Yanga hawana jambo lolote jipya zaidi ya kupenda kulalamika na kudai wameonewa. Na hivyo ndivyo itakavyotokea siku ya mchezo.
SWALI: Unazungumziaje kuhusu kusitishwa kwa adhabu ya kufungiwa kwa wachezaji watano wa Yanga, ambao walifungiwa kwa kosa la kumpiga mwamuzi Israel Nkongo wakati wa mechi yao dhidi ya Azam?
JIBU: Kwa kweli hakuna uamuzi mbovu na uliowashangaza mashabiki wa soka nchini kama huu uliotolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Nidhamu na Usuluhishi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Alfred Tibaigana. Kila mtu alikuwa shahidi wa tukio la wachezaji wa Yanga kumpiga mwamuzi, sasa hili la kutaka vielelezo limetoka wapi? Namheshimu sana kama yangu Tibaigana, lakini kwa hili naweza kusema amekosea.
Kwa mtazamo wangu, mtindo huu utazidi kudidimiza soka ya Tanzania kwa sababu wachezaji wetu wengi, hasa wa Yanga hawana nidhamu. Hivyo unapositisha adhabu iliyotolewa kwao, unawafanya wengine nao waone kumbe kumpiga mwamuzi ni jambo la kawaida.Nadhani huu ni woga tu wa baadhi ya wajumbe waliopo kwenye kamati ya Tibaigana kuona Yanga ikipokea kipigo kutoka kwa Coastal Union.
Tumekerwa sana na uamuzi huu na tutakachokifanya ni kuifunga Yanga ikiwa na kikosi chake chote ili viongozi, wanachama na mashabiki wake wakose cha kusema.
SWALI: Mbona umekuwa mkali sana kuhusu jambo hili?
JIBU: Unajua umefika wakati lazima tuseme ukweli. Hivi kuna nani ambaye hakuona kupitia vituo mbalimbali vya luninga jinsi wachezaji wa Yanga walivyofanya uwanjani katika mechi yao na Azam?.
Kwa kweli nawahurumia sana viongozi wenye nia ya kweli ya kuleta maendeleo ya soka nchini kwa jinsi wanavyotolewa maneno ya kashfa kutokana na kutenda haki.
Kila kukicha baadhi ya wadau wa soka nchini wamekuwa wakitoa lugha chafu kwa Rais wa TFF, Leodegar Tenga na viongozi wengine, wakiwemo Sunday Kayuni na Sadi Kawemba, lakini wanawaonea. Hawa watu wamekuwa wakiheshimu sheria za soka, lakini watu wengine wanawaangusha kwa makusudi.
SWALI: Nadhani ulikuwepo uwanjani na kushuhudia Simba ikiichapa ES Setif ya Algeria mabao 2-0 katika mechi ya michuano ya Kombe la Shirikisho iliyochezwa mwishoni mwa wiki iliyopita mjini Dar es Salaam. Una maoni gani kuhusu mchezo huo?
JIBU: Nimefurahishwa sana na ushindi walioupata Simba kwa sababu ni ushindi wa watanzania wote. Binafsi nawatakia maandalizi mazuri katika mechi yao ya marudiano. Lakini inabidi waende Algeria kwa tahadhari kubwa huku wakiwa na dhamira ya kuibuka tena na ushindi.
Nimefurahi kusikia kwamba kabla ya kwenda Algeria, watapitia Misri na kufanya mazoezi kwa siku kadhaa kwa lengo la kuzoea hali ya hewa ya huko. Hili ni jambo zuri sana katika maandalizi.
SWALI: Una maoni gani kuhusu ujio wa makocha wa kigeni hapa nchini? Unadhani wamekuwa wakitoa mchango wowote katika kukuza soka yetu?
JIBU: Kusema ukweli sio makocha wote wa kizungu waliotusaidia kukuza soka yetu. Kiwango chetu bado kimedumaa na wakati mwingine huwa naona ni bora makocha wazalendo wangepewa nafasi kwa kupelekwa nje kusomea mafunzo ya ukocha.
Wapo makocha wengi wazalendo hapa nchini wenye uwezo wa kuibua vipaji vya vijana na kuwaendeleza, lakini hawapati nafasi hiyo. Hawa makocha wa kigeni wanachotazama ni mechi za ligi tu, hawafiki mikoani, ambako ndiko kwenye vipaji vingi zaidi.
Binafsi napenda kumfagilia kocha wa sasa wa timu za Taifa za Vijana, Kim Poulsen kwa kupenda kusikiliza ushauri wa makocha wazalendo. Ndiye kocha pekee mzungu, ambaye yupo karibu na makocha wazalendo.

No comments:

Post a Comment