KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, March 22, 2012

DIAMOND: Sina demu, nipo singo



MSANII nyota wa muziki wa kizazi kipya, Naseeb Abdul ‘Diamond’ amesema kwa sasa yupo singo na kwamba hana papara ya kutafuta demu mwingine.
Diamond amesema ameamua kutulia kwa muda kwa sababu mapenzi hayapangwi, bali hutokea kimiujiza kama ilivyo kwa ajali ya aina yoyote.
Msanii huyo mwenye mvuto alisema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita kupitia kipindi cha Friday Night Live kilichorushwa hewani kupitia kituo cha televisheni cha Channel Five.
Diamond alisema kwa kipindi kirefu sasa, amekuwa akikumbana na mikasa mingi inayohusu mapenzi, hivyo ameamua kutulia na kumuomba Mungu ampatie mpenzi mwema.
Msanii huyo alielezea msimamo wake huo, kufuatia hivi karibuni kutengana na mpenzi wake wa siku nyingi, Wema Sepetu.
Mbali na Wema, Diamond pia amekuwa akidaiwa kuwa na uhusiano wa kimapenzi na wasanii wengi nyota wakiwemo Jokate Mwegelo na Irene Uwoya.
“Kusema ule ukweli, kwa sasa sina mtu, nipo singo. Na siwezi kusema nitapata mpenzi mwingine hivi karibuni kwa sababu siku zote mapenzi huwa yanapangwa, hayaji kama ajali,”alisema msanii huyo, ambaye kwa sasa anatamba na kibao chake cha Mawazo.
Alipoulizwa kuhusu kitu gani asichokipenda katika maisha yake ya usanii, Diamond alisema hapendi kuwaudhi mashabiki wake kwa vile wao ndio wanaomwezesha kuwa kwenye chati ya juu kimuziki.
Alisema siku zote amekuwa akijitahidi kubuni vitu vipya kwa ajili ya kuwaburudisha mashabiki wake na kusisitiza kuwa, msanii asipokuwa mbunifu, ni rahisi mashabiki kumchoka.
Diamond amemmwagia sifa kedekede prodyuza mahiri wa video za muziki nchini, Adam Juma kwamba ndiye aliyewainua wasanii wengi wa muziki wa kizazi kipya.
“Siku moja nilikaa mahali na Adam Juma nikamwambia, ‘bradha ikitokea siku ukasema unaacha kazi hii ama ikatokea Mungu amekuchukua mapema, wasanii tutapata tabu sana,’” alisema Diamond.
“Unaweza kutengeneza nyimbo ya kawaida, lakini ikabebwa na video. Adam ni mkali mno katika kutengeneza video za muziki wa kizazi kipya. Na video ndizo zinazoufanya muziki uonekane kuwa bora,”aliongeza.
Ili kwenda na wakati, Diamond alisema kwa sasa, ameamua kuwa na mbunifu wake wa mavazi, ambaye amekuwa akimtengenezea mavazi ya aina tofauti.
Alisema wasanii wanapaswa kuwa na mwonekano maalumu badala ya kuvaa mavazi yanayoweza kuwafanya waonekane wasela ama wahuni.
“Msanii hapaswi kuvaa nguo za makabitini. Wapo wasanii wengine wenye pesa na uwezo mkubwa, lakini hawapendi kuvaa, lakini ukishakuwa mtu maarufu katika jamii, unapaswa kubadilika,”alisema.

No comments:

Post a Comment