KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, March 1, 2012

Siwezi kuacha uigizaji filamu-Ini Edo



LAGOS, Nigeria
MCHEZA filamu tajiri wa kike nchini Nigeria, Ini Edo amesema kamwe hawezi kuachana na fani hiyo licha ya kufunga ndoa hivi karibuni.
Ini alisema mjini hapa wiki hii kuwa, licha ya kuishi mbali na mumewe, ndoa yao inakwenda vizuri na kila mmoja anaheshimu kazi ya mwenzake.
Mwanadada huyo mwenye sura na umbo jamali, alifunga ndoa mwaka jana na mfanyabiashara, Philip Ehiagwina wa Nigeria, ambaye anaishi Marekani.
“Nimeweza kuimiliki ndoa yangu,” alisema Ini. ‘Inategemea jinsi unavyoweka vipaumbele vyako na kuepuka vitu visivyokuwa na maana. Unapaswa kufahamu ni wakati gani unapaswa kuwepo mahali fulani na ni wakati gani hupaswi kuwepo mahali hapo.’
‘Ninachoweza kukifanya ni kuweka sawa maisha yangu ya kawaida na yale ya kikazi. Mume wangu anaishi Marekani, lakini tunakutana mara kwa mara. Aliondoka Nigeria Januari mwaka huu na mimi nitakwenda Marekani hivi karibuni, ‘ aliongeza.
‘Sifikirii iwapo nitaacha uigizaji. Naweza kujitosa katika kazi zingine, ambazo zinahusiana na filamu,’ alisisitiza mwanadada huyo.
Alipoulizwa kuhusu kashfa mbalimbali ambazo zimekuwa zikimuandama, Ini alisema mumewe anamfahamu vyema kuliko mtu mwingine yeyote.
‘Baadhi ya wakati wanapozungumza mambo kuhusu mimi, huwa tunakuwa pamoja. Hunitazama na kuniuliza kama mimi ni mtu yule yule, ambaye watu wanamzungumzia. Anaelewa nini ninachoweza kukifanya, ‘ alisema.
Ini alisema kamwe hajutii kuwa mwigizaji kwa vile fani hiyo imemwezesha kunufaika kimaisha. Alisema kwake, anajihisi amejaliwa kuwa na kipaji cha kazi hiyo.
‘Napenga uigizaji, licha ya mitazamo finyu kuhusu mimi. Sifikirii iwapo ningependa kufanya kitu kingine. Lakini baadhi ya wakati, ninakerwa na vitu vinavyoandikwa kuhusu mimi, hasa vikiwa vya uongo. Nimewahi kuchukua hatua za kisheria huko nyuma. Hiyo ndiyo njia pekee ya kupigania haki zetu,’ alisema.
Mwanadada huyo alisema anapenda kuendelea kuwa mwigizaji kwa kipindi kirefu kijacho na kuongeza kuwa, hata kama hatoigiza, ataendelea kuwa katika biashara hiyo.
Ini alianza kung’ara katika fani ya uigizaji mwaka 2000 na tangu wakati huo hadi sasa,ameshacheza filamu zaidi ya 50. Ni mwigizaji mwenye kipaji, akili na mzuri wa sura na umbo.
Hivi karibuni, Ini ambaye anayo shahada ya sanaa aliyoipata katika Chuo Kikuu cha Calabar, alizindua filamu yake ya kwanza inayojulikana kwa jina la I’ll take my chances.

No comments:

Post a Comment