KWA HABARI ZA MICHEZO NA BURUDANI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0719-153800 AU 0788-455808 AU EMAIL rashidzahor67@gmail.com '

Thursday, March 22, 2012

MILOVAN: LAZIMA WAARABU WAFE



SWALI: Tumeona jinsi kikosi chako kilivyokuwa kikichoka, hasa kipindi cha pili katika baadhi ya michezo ya hivi karibuni ya ligi kuu ya Tanzania Bara. Unaweza kutueleza tatizo ni nini?
JIBU: Ni kweli tatizo hilo lipo, nimeligundua na tayari nimeshaanza kulifanyiakazi ili kuhakikisha tunafanya vizuri katika mechi zetu zilizosalia za ligi kuu na ya Kombe la Shirikisho.
Yapo mambo mengi yaliyochangia hali hiyo, lakini kikubwa ni kwamba baadhi ya wachezaji wangu wamerejea uwanjani hivi karibuni baada ya kuwa majeruhi kwa muda mrefu.
Wachezaji kama Amir Maftah na Juma Jabu kwa sasa ni majeruhi na wakianza mazoezi baada ya kupona, wanaanza taratibu, hivyo wakipewa nafasi ya kucheza, wanachoka haraka kwa vile hawajafanya mazoezi ya nguvu kwa muda mrefu.
Tatizo hili limekuwa likinichanganya sana kwa sababu limekuwa likiiathiri timu kwa muda mrefu. Tatizo lingine ni ukosefu wa stamina kwa baadhi ya wachezaji. Lakini hili si kubwa na linaweza kurekebishika.
SWALI: Simba inatarajiwa kucheza na ES Setif ya Algeria Machi 25 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Je, umeshapata ripoti yoyote kuhusu wapinzani wenu?
JIBU: Kusema ukweli hadi sasa sijapata ripoti ya ES Setif, lakini tumefanikiwa kupata fununu kuhusu mbinu wanazotumia kimchezo katika mechi za nyumbani na ugenini. Wanatumia zaidi mfumo wa 4-5-1.
Nasi tumeshaanza kuutumia mfumo huu. Kama utakumbuka vizuri, tulicheza kwa kutumia mfumo huu katika mechi yetu dhidi ya Kagera Sugar na kushinda mabao 3-1. Pia tuliutumia katika mechi dhidi ya Toto African na kutoka nayo suluhu.
Lakini katika mechi yetu dhidi ya ES Setif hatutatumia mfumo huo muda wote wa mchezo. Tutaanza na mfumo wa 4-4-2 na baadaye kumalizia mfumo wa 4-5-1. Lengo letu ni kuwa na wachezaji wengi wa viungo ili kukabiliana na kasi ya mchezo na kucheza kwa kushambulia na kuzuia.
SWALI: Timu yako imekuwa ikipoteza nafasi nyingi za kufunga mabao kwenye michezo mbalimbali. Je umeshalifanyia kazi tatizo hilo kabla ya kucheza na ES Setif?
JIBU: Unajua tatizo la washambuliaji kushindwa kutumia vyema nafasi wanazopata kufunga mabao, halipo kwa Simba peke yake. Lipo kwenye timu nyingi, hata za Ulaya.
Hata hivyo, nimekuwa nikilifanyiakazi tatizo hilo mara kwa mara ili kuhakikisha timu yangu inaibuka na ushindi wa mabao mengi katika kila mechi zinazotukabili.
SWALI: Katika michuano ya ligi kuu msimu huu, tumeona baadhi ya timu zikiipania Simba? Unadhani ni kwa nini zinafanya hivyo?
JIBU: Simba ni timu kubwa na yenye rekodi nzuri katika ligi na michuano ya kimataifa. Vilevile katika michuano ya ligi kuu, kila timu imepania kutwaa ubingwa ikiwa ni pamoja na kuzishinda timu kongwe, hivyo ushindani wa aina hiyo lazima utokee.
Lakini kinachonisikitisha ni kwamba baadhi ya waamuzi wanaochezesha mechi za ligi wanashindwa kuheshimu sheria 17 za soka na wengine wanazikiuka kwa makusudi.
Wapo baadhi ya wachezaji wa timu pinzani, ambao wamekuwa wakiwaumiza wachezaji wangu kwa makusudi, lakini hakuna hatua zozote walizochukuliwa na waamuzi. Hali hii imechangia kwa kiasi kikubwa Simba kuwa na majeruhi wengi.
Uchezeshaji wa aina hii umekuwa ukizifanya baadhi ya klabu kuingia gharama kubwa za kuwatibu wachezaji wake na kuwakosa kwa muda mrefu kutokana na kuwa majeruhi.
Nadhani ni vyema waamuzi wawe makini katika kuwalinda baadhi ya wachezaji nyota, hasa wale wanaochezea timu ya taifa nap engine kutoa adhabu kali kwa wachezaji wenye tabia ya kucheza rafu za makusudi.
SWALI: Unawaeleza nini Watanzania kuhusu mechi yenu ya Jumapili na ES Setif ya Algeria?
JIBU: Nawaomba mashabiki wa soka wa Jiji la Dar es Salaam wajitokeze kwa wingi kushuhudia mechi hiyo kwa lengo la kuwaunga mkono wachezaji. Wakumbuke kwamba Simba ndio wawakilishi pekee wa Tanzania waliosalia katika michuano ya kimataifa, hivyo wanapaswa kuungwa mkono.
Pia nawaomba mashabiki wa Yanga waiunge mkono timu yetu badala ya kuizomea ama kuishangilia timu pinzani. Wanapaswa kuweka mbele uzalendo kwa nchi yao na kuacha ushabiki uliojaa chuki na uhasama usiokwisha.

No comments:

Post a Comment